Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 4 Public Service Management Ofisi ya Rais TAMISEMI. 33 2016-04-22

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:-
Suala la madai ya walimu nchini limekuwa ni tatizo sugu hususan kwa walimu wa shule za msingi na sekondari. Je, Serikali imechukua hatua gani ili kumaliza tatizo hilo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kulipa madeni yasiyo ya mishahara na mishahara kwa walimu walioko katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kila yanapojitokeza na kuhakikiwa. Aidha, mwezi Oktoba, 2015 Serikali ililipa madeni ya walimu yanayofikia shilingi bilioni 20.125 na mwezi Februari, 2016 imelipa jumla ya shilingi bilioni 1.17 ya madeni ya walimu nchini. Katika fedha za madai ya walimu zilizolipwa Oktoba, 2015 Mkoa wa Arusha ulipelekewa jumla ya shilingi milioni 504.6 ambapo kati ya hizo Halmashauri ya Wilaya ya Meru ilipokea jumla ya shilingi milioni 27.6 ambazo zilitumika kuwalipa walimu 716.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaendelea kukusanya madeni mapya ya walimu ambapo hadi tarehe 19 Aprili, 2016 madeni yasiyo ya mishahara yanafikia kiasi cha shilingi bilioni 17.5 kwa shule za msingi na sekondari wakati madeni ya mishahara yakifikia shilingi bilioni 49.8.
Mheshimiwa Naibu Spika, madeni haya yatafanyiwa uhakiki na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kisha kuwasilishwa Hazina ili yalipwe.