Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 50 2017-09-08

Name

Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Primary Question

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-
Manispaa ya Mtwara Mikindani ina migogoro mikubwa ya ardhi inayokaribia kusababisha uvunjifu wa amani:-
Je, Serikali ipo tayari hivi sasa kutatua migogoro hiyo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali Na. 50 la Mheshimiwa Mftaha Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa kumekuwepo changamoto ya kuibuka kwa migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara. Hata hivyo, Serikali imekuwa ikichukua hatua na jitihada mbalimbali ili kuhakikisha kuwa migogoro hiyo inapungua au inamalizika kabisa.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza azma hiyo, Wizara iliwataarifu Waheshimiwa Wabunge kuwasilisha taarifa za migogoro iliyopo katika maeneo yao. Aidha, Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya waliombwa kuwasilisha taarifa za mashamba makubwa yaliyotelekezwa na migogoro iliyopo katika mikoa yao kupitia barua yenye Kumb. Na. EA 171/438/01 ya tarehe 21 Desemba, 2015.
Mheshimiwa Spika, baada ya kupokea taarifa za migogoro kutoka katika maeneo mbalimbali, Wizara imekuwa ikiyapitia hayo na kutatua migogoro kama ilivyowasilishwa kutoka kwa viongozi wa maeneo husika.
Mheshimiwa Spika, kwa Mkoa wa Mtwara, Wizara ilipokea taarifa za migogoro mbalimbali ikiwemo migogoro mikubwa. Kati ya iliyopokelewa ilikuwa ni mgogoro wa Shamba la Chumvi, maarufu kama Libya; mgogoro wa Mjimwema na Tangila, maarufu kama UTT; mgogoro wa mipaka baina ya wakazi wa Mtepwezi na Jeshi la Magereza Lilungu; mgogoro kati ya wananchi wa Mangamba na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege; na mgogoro baina ya wananchi wa Mbae Mashariki na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Mheshimiwa Spika, kuhusu mgogoro katika eneo la Libya, wananchi walifikisha suala hilo Mahakamani na sasa shauri hilo lipo katika Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara kama Shauri la Madai Na. 7 la mwaka 2014. Kwa upande wa mgogoro wa UTT, mgogoro huu nao ulifikishwa Mahakamani kama Shauri la Madai Na. 8 la mwaka 2015 ambapo wananchi 723 wanadai fidia Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara na wapo tayari kuiondoa kesi hiyo Mahakamani endapo watalipwa fidia hiyo. Aidha, shauri hili litakuja Mahakamani kwa ajili ya usuluhishi wa mwisho tarehe 18, Septemba, 2017.
Mheshimiwa Spika, kwa maeneo mengine nchini ambayo yalitembelewa na timu ya wataalam wa kisekta iliyoundwa kuchunguza vyanzo vya migogoro ya ardhi na kupendekeza namna ya kuzitatua, Serikali itahakikisha kuwa migogoro yote inatatuliwa kwa wakati kwa kuzingatia mapendekezo yaliyotolewa.