Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 106 2017-09-15

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

RITTA E. KABATI aliuliza:-
Mwaka 2000 Serikali ilianzisha Mfuko wa Maendeleo ya Jamii ili kusaidiana na vyombo vingine vya Serikali kupunguza umaskini:-
Je, hali ya utekelezaji wa mpango huo wa TASAF ikoje?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali na Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilianzisha Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) mwaka 2000 ili kusaidiana na vyombo vingine vya Serikali kupunguza umaskini. Mafanikio makubwa yamepatikana katika awamu zote za utekelezaji kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa awamu ya kwanza ambayo ilitekelezwa mwaka 2000 hadi mwaka 2005 iliwezesha jamii kutekeleza miradi 1,704 yenye thamani ya shilingi bilioni sabini na mbili katika halmashauri 40 za Tanzania bara na wilaya zote za Tanzania Zanzibar. Miradi hiyo iliibuliwa na wananchi na ilihusisha sekta zote muhimu za afya, elimu, maji pamoja na barabara vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa awamu ya pili, TASAF ilitekelezwa mwaka 2005 hadi mwezi Juni, 2013 ambapo miradi 12,347 yenye thamani ya shilingi bilioni 430 katika halmashauri 126 za Tanzania Bara na wilaya zote za Tanzania Zanzibar. Miradi hii iliongeza upatikanaji wa huduma za maji, elimu, afya, pamoja na barabara vijijini na kuongeza upatikanaji wa chakula
Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya tatu ilizinduliwa mwaka 2012 na utekelezaji wake ulianza mwezi Januari, 2013 na unaendelea kutekelezwa hadi mwaka 2022 katika halmashauri 159 za Tanzania Bara na wilaya zote za Tanzania Zanzibar. Madhumuni ya TASAF awamu ya tatu ni kuwezesha kaya maskini kuongeza kipato, fursa pamoja na uwezo wa kuwagharamia mahitaji muhimu. Kazi zilizofanyika katika awamu ya tatu ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kaya maskini milioni 1.1 zenye jumla ya watu takribani milioni tano zimeandikishwa katika vijiji, mitaa na shehia 9,986. Hadi kufikia mwezi Agosti mwaka huu kaya hizi masikini zilishapokea ruzuku ya shilingi bilioni 521.9. Kaya hizo pia zimetekeleza miradi ya kutoa ajira za muda kwa kaya za walengwa 354,648 kutoka katika halmashauri 42 za Tanzania Bara pamoja na Tanzania Zanzibar. Hadi kufikia Agosti mwaka huu, jumla ya miradi 3,553 yenye thamani ya shilingi bilioni 51.1 kutoka katika vijiji 2,063, mitaa 329 na shehia 168 imeibuliwa na kutekelezwa. Hadi sasa miradi 2,952 imekamilika; lakini pia miradi 601 iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji kwa kukamilishwa katika mwaka huu wa fedha
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi Agosti mwaka huu, miradi ya kuendeleza miundombinu ya huduma za jamii 192 yenye thamani ya shilingi bilioni nane imetekelezwa Tanzania Bara na Zanzibar. Aidha, mpango wa kuhamasisha kaya kuweka akiba na kuwekeza unatekelezwa na umewawezesha walengwa kushiriki katika kuweka akiba katika vikundi na kutekeleza miradi ya ujasiriamali ikiwa ni mkakati endelevu wa kaya kutoka kwenye umaskini. Jumla ya vikundi 5,136 vya kuweka akiba na kuwekeza vyenye wanachama 11,907 vimeundwa katika Halmashauri sita za Tanzania Bara ambazo ni Kibaha, Bagamoyo, Chamwino, Lindi, Mtwara pamoja na Manispaa ya Lindi, Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.