Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 5 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 55 2017-09-11

Name

Dr. Joseph Kizito Mhagama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Madaba

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA aliuliza:-
Zaidi ya wananchi 181 wa kijiji cha Ngadinda Halmashauri ya Madaba wanalima ndani ya Wilaya ya Namtumbo kwa sababu ya kukosa eneo katika kijiji chao. Baraza la Madiwani lilishauri sehemu ya shamba la hekta 6,000 la Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi lililopo ndani ya kijiji hicho ambalo lilikabidhiwa kwa Halmashauri ya Wilaya ili litumike kwa shughuli za kilimo na sehemu ibaki kwa ajili ya mifugo. Hivi sasa wafugaji toka maeneo mbalimbali nchini wapo katika shamba hilo lakini wakulima hawajatengewa eneo.
(a) Je, Serikali haioni kwamba kitendo hicho ni ubaguzi na kinaweza kuchochea migogoro kati ya wafugaji na wakulima?
(b) Je, ni lini Serikali itasikiliza kilio cha muda mrefu cha wananchi wa Ngadinda cha kutengewa eneo la kilimo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Jimbo la Madaba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Songea mwaka 2014 iliunda Tume ya kuchunguza matumizi ya shamba hilo ambalo lilikuwa linamilikiwa na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na kubaini kuwa shamba hilo halitumiki vizuri kwa shughuli za ufugaji. Kwa msingi huo Tume ilipendekeza hekta 4000 wapewe wananchi wa Kijiji cha Ngadinda na eneo linalobaki la hekta 2000 libaki kwa shughuli za uwekezaji na ufugaji. Hata hivyo, baada ya Halmashauri ya Wilaya ya Wilaya ya Songea kugawanywa na kupata Halmashauri mpya ya Wilaya ya Mababa uamuzi huo haukutekelezwa. Hivyo, Halmashauri ya Madaba inatakiwa kujadili suala hili katika vikao vya Halmashauri na kufanya uamuzi kuhusu matumizi ya shamba hilo kwa kuzingatia maslahi ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyoelezwa katika sehemu (a) ya jibula msingi, Halmashauri ndiyo yenye jukumu la kujadili na kukubaliana kuhusu matumizi ya shamba hilo lililokuwa linatumika kwa shughuli za ufugaji. Serikali itatoa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha maslahi ya wakulima na wafugaji yanazingatiwa kuhusu matumizi ya shamba hilo.