Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 8 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 97 2017-09-14

Name

Eng. Joel Makanyaga Mwaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chilonwa

Primary Question

MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara inayounganisha Vijiji vya Msanga na Kawawa ni muhimu sana kiuchumi kwa Kata ya Msanga na Wilaya ya Chamwino na pia mazao mengi ya uhakika kutoka Kawawa na Vitongoji vyake lakini barabara hiyo ni korofi sana kwa sababu ya mbuga iliyopo kati ya vijiji hivyo viwili na daraja kubwa lililopo limevunjika kabisa kiasi kwamba halipitiki kabisa wakati wa mvua na wakati wa kiangazi hupitika kwa taabu sana.
Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha barabara hiyo na kulijenga daraja husika ili kuboresha mawasiliano ya vijiji hivyo viwili na masuala ya usafirishaji?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali katika mwaka wa fedha 2015/2016 ilitoa shilingi milioni 40 ambazo zimejenga kivuko (box culver) na kufungua mifereji ya kuitisha maji ya mvua (river draining). Aidha, mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetumia shilingi milioni 100 kuifungua barabara hiyo urefu wa kilomita 8, kujenga madaraja mbonyeo (solid drifts) matano likiwemo la mita 50 katika mto unaopitisha maji kutoka Hombolo na kuweka changarawe sehemu korofi kwa urefu wa kilomita 1. Serikali itaendelea kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino ili kuhakikisha daraja hilo linatengewa fedha na kujengwa katika mwaka wa fedha 2018/2019 kupitia TARURA.