Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 36 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 296 2017-05-29

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro wa ardhi kati ya Kampuni ya Highland Estate Mbarali na wananchi wanaolizunguka shamba hilo kwa kuwa mwekezaji amekuwa akipora ardhi kwa wananchi na kusababisha uvunjifu wa amani kwa muda mrefu sasa?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, shamba linalomilikiwa na Kampuni ya Highland Estate awali lilikuwa likimilikiwa na Shirika la Taifa la Kilimo na Chakula kuanzia mwaka 1978. Baada ya upimaji kukamilika 1981, shamba hilo liliendelea kumilikuwa na NAFCO kwa Hati Na. 327–DLR. Tarehe 18 Agosti, 2008 shamba hili liliuzwa na Serikali kwa Kampuni ya Highland Estate Ltd.
Mheshimiwa Spika, mgogoro wa shamba la Highland Estate unahusu tafsiri ya mipaka baina ya shamba hilo na vijiji vya Mwanavala, Ibumila, Imalilo, Songwe, Urunda, Ubaruku, Utyego, Mbarali, Mpakani, Mkombwe, Mwakaganga, Ibohola na Nyelegete.
Mheshimiwa Spika, hatua za awali za utatuzi wa mgogoro huu zinahitaji kupata tafsiri sahihi ya mpaka wa shamba kulingana na ramani ya upimaji iliyoidhinishwa na Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na vijiji vinavyozunguka shamba hilo. Zoezi la kutafsiri mipaka baina ya shamba na vijiji husika limeshaanza kufanyiwa kazi na wataalam wa Ofisi ya Mkuu wa wa Mkoa wa Mbeya, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mbarali pamoja na Ofisi ya Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kwa kushirikiana na wanakijiji husika isipokuwa wanakijiji wa kijiji cha Nyelegete ambao wamesusia zoezi hili.
Mheshimiwa Spika, juhudi za kutatua mgogoro huu bado zinaendelea kufanywa na Mkuu wa Wilaya ya Mbarali pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kwa kuwahimiza kijiji cha Nyalegete kutoa ushirikiano kwenye utatuzi wa mgogoro huu ili uweze kumalizika.
Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kutoa ushirikiano kwa wataalam wa sekta ya ardhi katika maeneo yao ili kuharakisha utatuzi wa migogoro ya ardhi hususan inayohusiana na mipaka ya mashamba. Aidha, napongeza Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kwa utaratibu wake wa kusikiliza kero za wananchi ikiwemo kutatua migogoro ya ardhi mara mbili kwa kila mwezi.