Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 30 2017-11-09

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Maboresho ya utendaji wa Serikali za Mitaa yalilenga kuimarisha na kujenga uwezo wa Serikali za Mitaa kujiendesha kwa kuwapatia rasilimali watu na fedha za kutosha kutekeleza Sera ya Ugatuaji wa Madaraka.
Je, Serikali ina lengo gani kuimarisha Serikali za Mitaa ziweze kujiendesha?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ibara za 145 na 146 za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mamlaka za Serikali za Mitaa ni mamlaka shirikishi za kisheria na kidemokrasia zilizoanzishwa kwa kwa lengo la kuwashirikisha wananchi katika shughuli zote za maendeleo, huduma za jamii, utawala bora, utekelezaji wa sheria, ulinzi na usalama kwa kuzingatia kanuni za uwazi na uwajibikaji.
Mheshimiwa Spika, tangu mwaka 1999 Serikali imetekeleza programu mbalimbali za kuboresha utendaji katika ngazi ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Miongoni mwa programu hizo ni Programu ya Maboresho ya Serikali za Mitaa iliyolenga kuimarisha miundo na mifumo ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ili zijiendeshe na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi. Aidha, Programu ya Maboresho ya Usimamizi wa Fedha imeimarisha na kuinua uwezo wa Halmashauri katika kukusanya mapato na kudhibiti matumizi.
Mheshimiwa Spika, katika kuziimarisha zaidi Mamlaka za Serikali za Mitaa, bajeti ya ruzuku ya maendeleo kwa Halmashauri imeongezeka kutoka shilingi bilioni 49 mwaka 2008 hadi shilingi bilioni 249 mwaka 2017. Aidha, kuanzia mwaka 2015, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeruhusiwa kwa mujibu wa sheria kuajiri watumishi wake wa kada 22 za ngazi za chini ikiwemo Watendaji wa Vijiji baada ya kupata kibali cha kuajiri. Ahsante.