Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 40 2017-11-10

Name

Yosepher Ferdinand Komba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y MHE. YOSEPHER F. KOMBA) aliuliza:-
Ni dhamira ya Serikali kutekeleza mpango wa elimu bure kuanzia chekechea hadi kidato cha nne, lakini mpango huu una changamoto ambazo zisipotatuliwa zitasababisha kushuka kwa ubora wa elimu.
(a) Je, ni nini tamko la Serikali juu ya wanafunzi wanaoanza kidato cha kwanza kwa kigezo cha kutofaulu kwa kiwango cha kianzia alama 100 na kuendelea?
(b) Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha ujenzi wa maabara unakamilika kwa wakati?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tamko la Serikali ni kwamba mwanafunzi anahesabiwa kufaulu mtihani wa Taifa wa darasa la saba endapo atapata alama kuanzia 100 hadi 250 katika masomo yote aliyoyafanya. Hata hivyo, wanafunzi walio na alama chini ya 100 huhesabika kuwa ni miongoni mwa waliokosa sifa za kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wanafunzi walioshindwa kufikia alama 100 na kuendelea, hushauriwa kujiunga na mfumo usio rasmi wa Elimu Masafa (Open Distance Learning) unaosimamiwa na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, vyuo vya ufundi au shule za sekondari za binafsi. Wanafunzi wanaojiunga na mfumo huo wa elimu hawamo katika utaratibu wa utekelezaji wa mpango wa elimu msingi bila malipo, lakini wanafunzi wanaosoma katika utaratibu huo watakaofaulu mtihani wa Taifa wa kidato cha nne huchaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la (b); ujenzi wa maabara katika Halmashauri zote unaendelea ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia masomo ya sayansi. Kati ya maabara 10,387 zinazohitajika nchini, ujenzi wa maabara 6,287 sawa na asilimia 60.5 ya mahitaji umekamilika.
Nazikumbusha Halmashauri zote kukamilisha mapema ujenzi unaoendelea kwa kushirikisha wadau na nguvu za wananchi.