Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 47 2017-11-10

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Katika mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa Mkoa wa Katavi uliofanywa na Halmashauri ya Mpanda mwaka 2004 kwa kushirikisha ngazi ya Mkoa na ngazi ya Wizara, zililipwa sehemu za Hifadhi za Misitu North East Mpanda (JB94) na Msanginia (JB215) na ramani mbalimbali kuidhinishwa ikiwemo 48870, 48893 na 40250.
Je, ni lini Serikali itabadili mipaka hiyo kwa mujibu wa Sheria ya Misitu ya 2002 (Namba 14) Kifungu cha 28?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuniwezesha kufika siku hii ya leo. Pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kuniamini na kuniteua katika nafasi hii. Tatu, nimshukuru Mheshimiwa Spika pamoja na uongozi mzima wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Wenyeviti wa Kamati nilizokuwa Mjumbe kwa malezi yao ambayo wameyatoa kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Misitu wa hifadhi wa Mpanda North East na Msangimya ni misitu ya Serikali inayosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania. Msitu wa North East Mpanda umehifadhiwa kwa tangazo la Serikali Na. 296 la mwaka 1949. Aidha, Msitu wa Msangimya umehifadhiwa kwa Tangazo la Serikali Na. 447 la mwaka 1954 na inasimamiwa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 Sura ya 323.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda ilipima maeneo ya Hifadhi ya Msitu wa Mpanda North East na Msangimya kupitia ufadhili wa Shirika la Africare chini ya mradi wa Ugalla Ecosystem ili kuanzisha maeneo ya usimamizi wa Wanyamapori (Wildlife Management Area- WMA) na makazi pamoja na kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya vijiji. Baada ya upimaji huo ramani 48870, 48893 na 40250 zilichorwa na Halmashauri husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya nia njema iliyokuwepo ya kuwapatia wananchi makazi yaliyopimwa kwa mujibu wa sheria na uanzishwaji wa maeneo ya usimamizi wa wanyamapori (WMA) na kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya kijiji, utaratibu huu haukuzingatia Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 pamoja na Sheria ya Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009. Kwa mujibu wa kifungu cha 31(1) cha Sheria ya Wanyamapori, WMA zote zinaanzishwa kwenye misitu iliyoko kwenye ardhi ya kijiji au ardhi ya ujumla na siyo kwenye misitu ya Hifadhi ya Serikali Kuu. Aidha, mpango wa matumizi bora ya ardhi ya kijiji inafanyika kwenye ardhi ya kijiji husika na siyo kwenye misitu iliyohifadhiwa kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ardhi ya msitu wa hifadhi uweze kutumika kwa matumizi mengine, Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 katika kifungu cha 29 inatoa utaratibu wa kisheria wa kufuta hadhi ya msitu wa hifadhi ambapo Waziri wa Maliasili na Utalii anaweza kufuta sehemu ya msitu au msitu wote wa hifadhi baada ya kujiridhisha kuna umuhimu ya kufanya hivyo. Mara baada ya mchakato huu kukamilika ndipo ardhi ya msitu itatumika kwa matumizi na shughuli zingine za kibinadamu mbali na uhifadhi. Aidha, Waziri wa Maliasili na Utalii atatoa maamuzi hayo baada ya kushauriana na Kamati ya Taifa ya Ushauri wa Misitu (National Forestry Advisory Committee) ambayo inatajwa katika Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 katika Kifungu cha 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mchakato wa kupima sehemu ya misitu ya hifadhi niliyoeleza hapo juu umefanyika kinyume cha sheria na taratibu zilizopo, hadhi ya misitu hiyo ya hifadhi inaendelea kubaki kisheria kama ilivyoainishwa kwa mujibu wa matangazo ya Serikali niliyoyataja hapo juu. Aidha, Serikali itaangalia kama kunaweza kuwa na uwezekano wa maeneo hayo kutolewa kwa ajili ya matumizi mengine kwa mujibu wa sheria, lakini ikiweka kipaumbele kwanza kitatolewa kwa maslahi mapana ya Taifa na kwa kufuata ushauri utakaotolewa na Kamati ya Taifa ya Ushauri ya Misitu.