Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 49 2017-11-10

Name

Amb. Adadi Mohamed Rajabu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muheza

Primary Question

MHE.BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-
Vitalu vya miti ya tiki – Lunguza Muheza huuzwa kwa njia ya mnada hali inayosababisha viwanda vidogo vidogo vya Muheza kukosa miti.
(a) Je, ni lini Serikali itahakikisha wenye viwanda katika maeneo hayo wanapata vitalu ili kulinda ajira za wanavijiji?
(b) Je, kwa nini wanaopata vitalu wasichane magogo hayo hapo Wilayani ili kulinda viwanda vidogo vidogo vya Muheza?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza lenye sehemu na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye biashara ya miti ya misaji, njia mbili ambao ni mnada na makubaliano binafsi hutumika. Mbinu mbalimbali zimekuwa zikitumika katika kuuza miti ya misaji ili kuongeza bei ya miti kwa kutumia ushindani wa bei iliyopo sokoni. Hivyo, ili kupata bei ya soko, mbinu inayotumiwa ni pamoja na kuuza kiasi kidogo cha ujazo wa miti ya kuvuna kwa njia ya mnada. Hivyo, asilimia 30 ya malighafi inayotarajiwa kuvunwa katika shamba husika huuzwa kwa utaratibu huu. Njia hii inasaidia kubaini nguvu ya soko na kuongeza mapato ya Serikali. Njia ya makubaliano binafsi hutumika pia katika uuzaji wa miti mara baada ya bei ya soko kupatikana katika mnada. Hivyo asilimia 70 huuzwa kwa makubaliano binafsi ili kutoa fursa kwa wadau wengi zaidi kushiriki kwenye biashara hiyo. Utaratibu huu kwa kiasi kikubwa umewawezesha wenye viwanda wanaoshindwa kununua kupitia njia ya mnada kupata malighafi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza wigo wa soko la ndani, Wizara imeanzisha utaratibu utakaowawezesha wanunuzi wengi wa miti ya misaji walioko nchini kunufaika. Utaratibu huu unawalenga wale wote wenye viwanda vinavyotengeneza samani vilivyopo nchini. Hivyo, katika mwaka wa fedha 2017/2018 asilimia 10 kati ya asilimia 70 ya ujazo wa miti uliotengwa kwa ajili ya kuuzwa kwa njia ya makubaliano binafsi utauzwa kwa watengenezaji wa samani ndani ya nchi ili kuongeza thamani ya mazao yao na kuongeza ajira. Matangazo ya mauzo ya miti hufanyika kwa kubandika katika mbao za matangazo na kutolewa katika magazeti kwa muda wa siku 14 kabla ya mauzo. Wenye nia ya kuvuna na wenye kumiliki mashine za kupasua magogo ikiwemo wana vijiji wanaozunguka shamba letu la miti la Mtibwa na Longuza hupewa matangazo hayo kuhusu mnada huo ili nao waweze kujitokeza katika kununua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kulinda viwanda vya ndani na kuongeza ajira kwa Watanzania, uchakataji wa magogo yanayovunwa katika mashamba ya miti hufanyika ndani ya nchi. Baada ya kuuziwa malighafi kutoka katika mashamba ya miti, uchakataji hufanywa na mteja mwenyewe kulingana na mahali alipoweka kiwanda chake. Sheria na mwongozo wa uvunaji wa mazao ya misitu haimlazimishi mwenye kiwanda kujenga kiwanda mahali malighafi inapopatikana.
Nashauri Waheshimiwa Wabunge, tuendelee kuhimiza Halmashauri zetu ziweke mazingira wezeshi kwa wawekezaji wa viwanda vidogo na vikubwa katika maeneo yaliyo karibu na mashamba ya miti ili kuongeza ajira kwa wananchi wanaoishi karibu na mashamba hayo.