Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 14 2018-01-30

Name

Raphael Michael Japhary

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. RAPHAEL J. MICHAEL aliuliza:-
Je, Serikali imejipanga vipi kumaliza madai ya msingi na ya muda mrefu kwa waongoza watalii, wapagazi na wapishi kutambuliwa kwa kima cha chini cha mishahara, mikataba ya kazi inayoendana na kazi zao, malipo ya posho kwa huduma wanazotoa kwa siku, sera shirikishi katika kutatua matatizo yao na utalii wa nchi kwa ujumla na malipo ya huduma za jamii kama vile afya na majanga?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII MAJIBU alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Raphael Japhary Michael, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, madai ya wapagazi, wapishi na waongoza watalii yameshughulikiwa na Wizara kwa kushirikiana na Vyama vya Tanzania Association of Tour Operators (TATO); Kilimanjaro Association of Tour Operation (KIATO); Tanzania Tour Guides Association (TTGA); Kilimanjaro Guides Association (KGA); Tanzania Porters Organization (TPO); Ofisi ya Waziri Mkuu, (Kazi Ajira, Vijana na Ulemavu) na Vyama vya Wapagazi na Wapishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkutano uliofanyika Arusha tarehe 12 Desemba, 2015 Wizara na wadau walikubaliana kuhusu viwango vya chini vya ujira kwa wapagazi wapishi na waongoza watalii. Viwango vinavyopendekezwa kwa siku ni shilingi sawa na dola za Marekani 10 kwa wapagazi 15; kwa wapishi na 20 kwa waongoza watalii kwa siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika makubaliano hayo, Serikali ilisisitiza juu ya umuhimu wa kuingia mikataba ya kazi baina ya waajiri na waajiriwa. Serikali ilitoa miongozo ya mikataba ili izingatiwe kwa mujibu wa matakwa ya kila kundi na ilianza kutumika katika Sekta ya Utalii. Waajiri na wajiriwa wanatakiwa kisheria kutekeleza wajibu wao wa kusaini mikataba na kuzingatia viwango vilivyokubaliwa. Endapo makubaliano yao hayatazingatiwa, ni wajibu wa waajiriwa kutoa taarifa kwenye mamlaka husika za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kima cha chini cha mishahara na malipo ya posho kwa huduma za jamii kama vile afya na majanga, Serikali inaendelea kuhimiza kuwa waajiri wazingatie kima cha chini cha mishahara kilichotolewa na Serikali na michango inayopaswa kutolewa kwenye mifuko mbalimbali kama vile Shirika la Taifa la Hifadhi wa Jamii (NSSF), Bima ya Afya na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi.