Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 11 2018-04-04

Name

Ester Alexander Mahawe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-
Takwimu zinaonesha upungufu mkubwa wa matundu ya vyoo zaidi ya 200,000 katika shule mbalimbali za sekondari na msingi.
(a) Je, nini mkakati wa Serikali wa kumaliza tatizo hilo?
(b) Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kuja na mkakati mbadala kama ilivyofanya wakati wa kumaliza tatizo la madawati na maabara nchini?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tuna upungufu wa matundu ya vyoo 276,198 kwa shule za msingi na 20,534 kwa shule za sekondari. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya matundu ya vyoo 6,708 kwa shule za msingi na 2,071 kwa shule za sekondari yamejengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya tathmini ya kina tumebaini kuwa zinahitajika jumla ya shilingi bilioni 646.822 kumaliza tatizo hilo. Wizara yangu imetoa maelekezo kwa halmashauri zote kwamba katika Bajeti ya mwaka 2018/2019, fedha za ruzuku ya maendeleo ambazo ni jumla ya shilingi bilioni 55.2 endapo zitapitishwa na Bunge, sehemu kubwa ya fedha hizo ielekezwe kwenye kipaumbele cha miundombinu ya elimu ikiwemo vyoo kwenye shule zote ambazo tayari wananchi watakuwa wamechangia nguvu zao.
Uamuzi huo utatoa nyongeza kubwa sana kwenye Bajeti ya shilingi bilioni 19.97 ambayo imetengwa chini ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mahsusi kwa ajili ya matundu ya vyoo katika shule za msingi na shule za sekondari. Mkakati wa Serikali ni kutumia fedha hizo kumalizia kazi za ujenzi ambazo zitakuwa zimeanzishwa na wananchi.