Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 42 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 343 2017-06-06

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Kijiji cha Nyakanazi, Wilaya ya Biharamulo kiko kwenye njia panda kwenda Kigoma, Kahama, Ngara na kina wakazi wapatao 15,000. Kulingana na hali hiyo, kuna shughuli nyingi za kiuchumi zinaibuka na idadi ya watu inaongezeka kwa kasi; aidha, kijiji hicho pia kimebanwa na hifadhi inayopakana nacho.
Je, Serikali ipo tayari kujadiliana na Halmashauri ya Wilaya na wakazi wa Nyakanazi ili kuona uwezekano wa upanuzi wa eneo la kijiji kwa upande wa hifadhi inayopakana na kituo cha polisi kwa nia ya kufungua fursa za kiuchumi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Hifadhi za Taifa ya mwaka 2002 Sura Na. 282, shughuli za makazi, ufugaji, kilimo na shughuli nyingine za kibinadamu huwa haziruhusiwi isipokuwa kama Wizara yenye dhamana ya Maliasili na Utalii itaruhusu kwa kibali maalum.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, endapo ardhi ya Nyakanazi haitoshelezi mahitaji, kijiji kinapaswa kuwasilisha maombi ya ardhi ambayo yatajadiliwa katika vikao vya Halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa ili kupata ufumbuzi. Maoni hayo yatawasilishwa Wizara ya Maliasili na Utalii na endapo Wizara hiyo yenye dhamana itaridhia upanuzi wa eneo hilo la kijiji, basi unaweza kufanyika.