Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 43 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 359 2017-06-07

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-
Ardhi ikipimwa huwa na thamani na hivyo kuwafanya wamiliki kupata mikopo katika taasisi za kifedha na kuwekeza katika uchumi. Katika Jimbo la Tarime Mjini ni Kata mbili tu za Bomani na Sabasaba ndizo ambazo ardhi yake imepimwa kwa asilimia 75 kati ya kata nane zilizopo, hii inatokana na upungufu mkubwa wa wataalam wa kupima ardhi.
Je, ni lini Serikali itapeleka wataalam wa kutosha ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tarime kuweza kupima ardhi kwa kata sita zilizosalia ili wananchi wa Tarime Mjini waweze kunufaika na ardhi yao?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, swali lake Na. 359 kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kupanga na kupima ardhi nchini kwa manufaa ya wananchi wake. Halmashauri ya Mji wa Tarime ina wataalam wa ardhi wanne tu ambao ni Afisa Mipango Miji, Afisa Ardhi, Mchora ambaye ni Mrasimu Ramani na Mthamini Mali. Idadi hii ni ndogo ukilinganisha na kasi ya ukuaji wa Mji wa Tarime kwa sasa. Tatizo hili si kwa Mji wa Tarime pekee bali ni tatizo linalozikabili karibu Halmashauri zote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na hali hiyo, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ili kutekeleza azma ya kupanga na kupima kila kipande cha ardhi kwa nchi nzima, ikiwemo kusajili makampuni binafsi ya kupanga ardhi, yenye weledi wa kufanya kazi hiyo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo. Hadi sasa tuna jumla ya makampuni 36 ya kupanga miji na makampuni 65 ya kupima ardhi yamesajiliwa ili kuongeza kasi ya upangaji na upimaji wa ardhi nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa inaandaa utaratibu wa kuwatumia wataalam wa sekta ya ardhi kutoka katika maeneo yenye watumishi wa kutosha kufanya kazi katika maeneo yenye uhaba mkubwa wa watumishi na hivyo kuharakisha kasi ya upangaji na kupima ardhi nchini. Halmashauri ya Mji wa Tarime ni mojawapo ya maeneo yanayotarajiwa kunufaika na utaratibu huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu pia inaendelea kuzihimiza Halmashauri zote nchini kutenga fedha za kutosha katika bajeti zao kwa ajili ya kuajiri wataalam wa sekta ya ardhi wanaokidhi mahitaji na hivyo kuongeza kasi ya kupanga na kupima ardhi katika maeneo yao.