Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 8 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 69 2016-04-29

Name

Yahaya Omary Massare

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Magharibi

Primary Question

MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza:-
Ili Mtu au Kampuni iweze kufanya biashara ya Mazao ya Misitu anapaswa kusajiliwa:-
(a) Je, ni kwa nini usajili huu hufanywa kila mwaka?
(b) Je, Serikali haioni kwa kufanya hivyo kunaongezea walipa kodi mzigo?
(c) Je, usajili huu hauwezi kufanywa pale tu mtu au Kampuni inapoanza biashara kwa mara ya kwanza na anapoendelea aweze kuhuisha badala ya kusajiliwa upya kila mwaka.

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, lenye sehemu (a), (b) na (c), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, usajili wa wafanyabiashara wa mazao ya misitu hufanywa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Sura 323, kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, Kifungu cha tano (5) na Kifungu cha 108 na Kanuni zake za mwaka 2004, Kanuni ya 54 kwa kuzingatia kiasi cha mazao ya misitu cha kuvuna mwaka hadi mwaka, ambacho hutegemea uwezo na ndicho kigezo cha kutambua idadi ya wafanyabiashara wa mazao ya misitu watakaopewa vibali vya kuvuna ili kuepuka kuwa na idadi kubwa ya wateja kuliko uwezo wa msitu kuvunwa katika mwaka husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, usajili wa kila mwaka husaidia kutekeleza mipango endelevu ya usimamizi kwa ajili ya kupanga kiwango kinachotakiwa kuvunwa kwa mwaka. Aidha, utaratibu huu hutoa fursa kwa wafanyabiashara wapya kuingia kwenye soko hivyo kuweka mipango mizuri zaidi ya kutambua mahitaji yao kulinganisha na uwezo wa misitu iliyopo. Vile vile kutoa fursa kwa wananchi wengi zaidi kushiriki na kunufaika na uvunaji wa rasilimali za Taifa, mazao ya misitu ikiwa ni sehemu yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa zoezi la usajili huambatana na ada mahsusi, wafanyabiashara waone kuwa hii ni fursa kwao kuchangia pato la Taifa kupitia biashara wanazozifanya, utaratibu ambao unafanana na masharti ya biashara nyingine zinazofanyika hapa nchini.