Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 4 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 28 2018-04-06

Name

Issa Ali Abbas Mangungu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbagala

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI (K.n.y. MHE. ISSA A. MANGUNGU) aliuliza:-
(a) Je, Mabaraza ya Wazee katika Mahakama za Mwanzo yapo kwa mujibu wa sheria?
(b) Mahakama ya Mwanzo Kizuiani hulipa posho za Wazee wa Baraza kiasi cha shilingi 5,000 kila wanapomaliza shauri. Je, kwa nini sasa yapata miezi tisa wazee katika Mahakama ya Mwanzo Kizuiani hawajalipwa posho zao?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya Wazee wa Mahakama nchini yamehalalishwa na sheria. Kifungu cha 9(1), (2) na (3) cha Sheria ya Mahakama za Mahakimu, Sura ya 11 ya sheria za nchi kinaeleza kuwa kutakuwa na matumizi ya Wazee wa Mahakama katika Mahakama ya Mwanzo na Mahakama za Wilaya na Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mahakama ya Mwanzo ya Mbagala kama ilivyo katika Mahakama nyingine, malipo ya posho za Wazee wa Baraza yamekuwa yakipewa kipaumbele kulingana na upatikanaji wa fedha. Malipo haya yamekuwa yakifanyika kwa mkupuo wa miezi mitatu au minne ili kutoa fursa ya kuweka kumbukumbu za malipo baada ya mchakato wa kukokotoa malipo stahiki kwa kila mlipwaji kulingana na idadi ya mashauri yaliyomalizika ambayo mhusika ameshiriki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2016/2017 Wazee wa Mahakama zote za Mwanzo katika Mkoa wa Dar es salaam ikiwemo Mahakama ya Mwanzo Mbagala walilipwa posho zao zote. Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Wazee wa Baraza katika Mahakama ya Mwanzo Mbagala wameshalipwa posho zao kwa kipindi cha Julai hadi Novemba, 2017 kiasi cha shilingi 5,760,000. Vilevile kiasi cha shilingi 2,840,000 ambacho ni madai ya wazee hao kwa kipindi cha Desemba, 2017 hadi Februari, 2018, kipo katika mchakato wa malipo na hivyo hakutakuwa na deni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutoa umuhimu wa kipekee katika malipo ya posho ya Wazee wa Baraza ili kutokwamisha mashauri yaliyopo Mahakamani hususan kwa Mahakama za Mwanzo.