Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 8 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 70 2016-04-29

Name

Risala Said Kabongo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MEH. RISALA S. KABONGO aliuliza:-
Utekelezaji wa Tangazo rasmi la Serikali la Mwaka 2008 juu ya mpaka mpya wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha katika Bonde la Usangu umeshindikana, hivyo kufanya upanuzi holela wa maeneo ya kilimo, uvamizi wa mifugo mingi na matumizi holela ya maji katika kilimo, jambo ambalo limesababisha uharibifu wa mazingira, Mto Ruaha Mkuu kuendelea kukauka kila mwaka na kuathiri uzalishaji umeme katika Bwawa la Mtera na Kidatu na shughuli zingine na matumizi ya maji ya Mto Ruaha Mkuu:-
(a) Sababu zipi za msingi zilizosababisha utekelezaji wa Tangazo hilo kushindwa kwa takribani miaka nane sasa?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani za haraka ili kunusuru na kusitisha uharibifu mkubwa wa mazingira unaoendelea katika Bonde la Usangu?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Risala Said Kabogo, Mbunge wa Viti Maalumu, lenye Sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inampongeza Mheshimiwa Risala Kabongo kwa kutambua na kuthamini jitihada za Serikali na kuona umuhimu wa uhifadhi katika Taifa, hususan uhifadhi katika eneo la Hifadhi ya Taifa ya Ruaha katika Bonde la Usangu, ambako shughuli za kilimo, uingizaji, uchungaji na ulishaji mifugo na matumizi ya maji yasiyo endelevu katika kilimo zimesababisha uharibifu mkubwa wa mazingira, unaosababisha pamoja na athari nyingine kukauka kila mwaka kwa Mto Ruaha Mkuu na hatimaye kuathirika shughuli za uzalishaji umeme kutokana na kukosekana kwa kiasi cha maji kinachohitajika katika mabwawa ya Mtera na Kidatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia umuhimu nilioainisha hapo juu Serikali ilikamilisha taratibu zote husika na kutoa Tangazo la Serikali Namba 28 la mwaka 2008, ambalo msingi wake ni Sheria ya Hifadhi za Taifa, Sura ya 282, hususan Kifungu cha tatu (3) na cha nne (4) cha sheria hiyo ili eneo la Bonde la Usangu lijumuishwe ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha.
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Tangazo la Serikali Namba 28 la mwaka 2008 haujashindikana na badala yake matakwa ya Tangazo hilo yameanza kwa kuhakiki mipaka na kuweka alama za kudumu beacons kwa baadhi ya maeneo yaliyoongezwa. Kutoa elimu na kuhamasisha wananchi waliotakiwa kuhama ili kupisha hifadhi, kufanya tathmini na kulipa fidia ya ardhi na mali zisizohamishika kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Na. 4 na Na. 5 za mwaka 1999. Aidha, Serikali inaendelea na utekelezaji wa matakwa ya Tangazo la Serikali Namba 28 la mwaka 2008, ambapo baada ya changamoto zilizojitokeza kutatuliwa, wananchi walioko katika eneo husika pamoja na mali zao zinazohamishika wataondoka kupisha shughuli za uhifadhi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu yangu ya swali Namba 53 lililouliza na Mheshimiwa Haroon Mulla Pirmohamed, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, katika Kikao cha Sita cha Mkutano wa Tatu wa Bunge la Kumi na Moja kilichofanyika tarehe 27/4/2016, nilisisitiza kuhusu umuhimu wa kuhifadhi eneo la Bonde la Usangu kwa maslahi mapana ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu hayo nilieleza kuhusu kuwepo kwa timu ya Wataalam iliyopitia changamoto za utekelezaji wa Tangazo la Serikali, ikiwa ni pamoja na kutafsiri mpaka, kuweka alama na kukamilisha malipo ya fidia kwa mujibu wa sheria katika kipindi cha mwezi mmoja, hatua ambayo itawezesha Serikali kuendelea na hatua muhimu na za haraka ili kudhibiti uharibifu wa mazingira katika Bonde la Usangu.