Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 10 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 85 2018-04-16

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Primary Question

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE aliuliza:-
Maeneo mengi ya Halmashauri ya Chalinze yamefaidika na Mradi wa REA Awamu ya Pili lakini katika utekelezaji wa mradi huo Miji ya Kiwangwa, Hondogo, Mkange na Kibindu bado haijafikiwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuifikia miji hiyo?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Kiwangwa katika Jimbo la Chalinze umepatiwa umeme kupitia mradi uliotekelezwa na TANESCO kwa ufadhili wa Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) awamu ya kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ulishakamilika na wateja zaidi ya 600 wameunganishiwa umeme. Kijiji cha Hondogo kimepatiwa umeme kupitia mradi wa densification awamu ya kwanza uliokuwa unatekelezwa na Mkandarasi Kampuni ya STEG international Services kutoka Tunisia. Kazi za mradi huu zimegharimu shilingi bilioni 1.16 ambapo wateja zaidi ya 66 wameunganishiwa umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Mkange kitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Peri Urban utakaotekelezwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia za umeme wa msongo wa kilovolt 33 wenye urefu wa kilometa 26 kutoka Miono hadi Saadani utakaonufaisha Vijiji vya Manda, Mazingara na Gongo. Gharama za kuvipatia umeme vijiji hivi ni shilingi bilioni tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Kibindu kitapatiwa umeme kupitia njia ya umeme ya msongo wakilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 66 kutoka shule ya sekondari Changarikwa. Njia hii ya umeme itanufaisha pia vijiji vya Kwaruhombo, Kwamduma, Kwamsanja na Kwankonje. Gharama ya kufikisha umeme katika vijiji hivi ni shilingi bilioni tano. Kazi hizi zitatekelezwa kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu, mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwaka 2021. Ahsante. (Makofi)