Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 14 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 113 2018-04-20

Name

Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. QAMBALO W. QULWI aliuliza:-
Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kuwa ardhi yote ya Tanzania inapangwa, inapimwa na kumilikishwa kisheria kama namna mojawapo ya kuondoa migogoro hususan ya wakulima na wafugaji nchini?

Name

William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Answer

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Qambalo Willy Qulwi, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kupanga na kupima ardhi yote nchini kama namna mojawapo ya kupunguza migogoro baina ya watumiaji wa ardhi, hususan wakulima na wafugaji na watumiaji wengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi Na. 6 ya Mwaka 2007, uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi ni jukumu la mamlaka ya upangaji ambazo ni halmashauri za wilaya na vijiji. Aidha, kifungu cha 7(1) cha Sheria ya Mipangomiji Na. 8 ya Mwaka 2007 kinaelekeza kuwa jukumu la upangaji na uendelezaji miji lipo chini ya mamlaka za upangaji ambazo ni Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji, Wilaya na Mamlaka za Miji Midogo. Wizara yangu imekuwa ikizihamasisha na kuzijengea uwezo mamlaka za upangaji katika kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi na kuandaa mipango kabambe ambayo ndiyo dira ya kuongoza uendelezaji wa ardhi katika maeneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha kuwa ardhi yote ya Tanzania inapangwa, inapimwa na kumilikishwa kisheria. Mikakati hiyo ni pamoja na kuandaa Programu ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha kila Kipande cha Ardhi Nchini ambayo itahusisha halmashauri zote nchini; kusajili makampuni binafsi ya kupanga na kupima ardhi yenye weledi wa kufanya kazi hizo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo na kununua vifaa vya kisasa vya upimaji vitakavyosambazwa kwenye kanda nane za usimamizi wa ardhi kwa lengo la kuharakisha upimaji wa ardhi katika wilaya mwaka huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa suala la upimaji wa ardhi ni endelevu, natoa rai kwa halmashauri zote nchini kutenga fedha za kutosha katika bajeti zao kila mwaka kwa ajili ya kurahisisha na kuharakisha zoezi la kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi na mipango kabambe na hivyo kuwezesha kukamilika kwa azma ya kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi nchini kwa wakati.