Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 16 Energy and Minerals Wizara ya Madini 127 2018-04-24

Name

Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Primary Question

MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-
Katika Mji wa Tunduru yako mabango mengi yanayoelezea ununuzi wa madini jambo linaloashiria upatikanaji mkubwa wa madini kutoka kwa Wachimbaji wadogo wadogo ambao hawatambuliwi kwa mujibu wa sheria:-
Je, ni lini Serikali itawatengea maeneo ya kuchimba madini na kuwatambua Kisheria Wachimbaji hao wadogo wadogo?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. DOTTO M. BITEKO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini na kabla sijajibu swali hili naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Profesa Idris Kikula kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Tume mpya ya Madini.
Mheshimiwa Spika, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2017 inawatambua wachimbaji wadogo. Kwa kutumia sheria hiyo Serikali inatoa leseni za uchimbaji za madini (Primary Mining Licenses) kwa ajili ya wachimbaji wadogo.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa kuna mabango na maduka mengi yanayotangaza uwepo wa madini ya vito katikati ya Mji wa Tunduru huko Mkoani Ruvuma. Baadhi ya madini ya vito hayo yaliyopo Wilaya ya Tunduru ni pamoja na Sapphire, Ruby, Garnet na kadhalika. Maduka ya madini yenye mabango ni ya wafanyabiashara wakubwa wenye leseni kubwa (Dealers License) ambazo huhuishwa kila mwaka kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Spika, mwaka 2013 Serikali ilitenga eneo la Mbesa, Wilaya ya Tunduru, lenye ukubwa wa hekta 15,605.3 kwa tangazo la Serikali Namba tano la tarehe 22 Februari, 2013, kwa ajili ya uchimbaji mdogo wa madini ya shaba. Hadi Aprili, 2018 jumla ya leseni hai 649 za wachimbaji wadogo wa madini yaani (PML) zimetolewa Wilaya ya Tunduru.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo kadri taarifa za utafiti katika maeneo hayo zitakavyoandaliwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kwa kushirikiana na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ili wachimbaji wadogo hao waweze kuchimba madini siyo kwa kubahatisha.
Mheshimiwa Spika, aidha, wachimbaji wadogo wanahimizwa kuomba leseni ili wafanye shughuli za utafutaji wa madini kwa mujibu wa sheria za nchi ili kuinua vipato vyao kutoa ajira kwa Watanzania, kuchangia pato la Taifa kupitia tozo mbalimbali zinazotokana na shughuli za madini.