Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 20 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 171 2018-05-02

Name

Prof. Norman Adamson Sigalla King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Primary Question

MHE. PROF. NORMAN S. KING aliuliza:-
Hifadhi ya Kitulo iliyoko Mkoa wa Njombe, Wilaya ya Makete ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu na ni hifadhi ya kipekee katika Afrika kwa sababu ina aina tofauti ya maua zaidi ya 120.
Je, ni lini TANAPA kwa kushirikiana na TANROADS itaona umuhimu wa kujenga kwa lami barabara ya kutoka Chimala – Matamba – Kitulo – Makete ili kurahisisha uingiaji wa watalii kwenye mbuga hiyo?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Norman Sigalla King, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakubaliana na hoja ya Mheshimiwa Mbunge kwamba, kujenga barabara ya Chimala – Matamba – Kitulo kwa kiwango cha lami ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu na hasa jamii zitakazotumia barabara hiyo ikiwa ni pamoja na hifadhi ya Kitulo. Napenda kuchukua fursa hii kumwarifu Mheshimiwa Mbunge kuwa kwa hivi sasa Wizara yangu ina mchakato wa kuboresha miundombinu ya barabara, utalii na utawala kwenye hifadhi zetu, mojawapo ikiwa ni Hifadhi ya Kitulo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu la ujenzi wa barabara zilizo nje ya hifadhi ni jukumu la Halmashauri za maeneo husika ikishirikiana na TANROADS. Kutokana na hali halisi ya mapato ya Shirika la Hifadhi ya Taifa, Hifadhi ya Taifa haina uwezo wa kuchangia ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami, kama alivyoomba Mheshimiwa Mbunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto hiyo, Wizara yangu itaendelea kushirikiana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili barabara hiyo iwekwe kwenye mpango wa ujenzi wa lami. (Makofi)