Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 23 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 188 2018-05-07

Name

Ally Seif Ungando

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibiti

Primary Question

MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-
Ufunguzi wa Kituo cha Afya Mbwera ulifanyika tarehe 27/8/1994 na aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, wakati huo Dkt. John Samwel Malecela lakini hadi sasa kituo hicho hakina hadhi hiyo ya kuitwa Kituo cha Afya.
(a) Je, Mheshimiwa Waziri mwenyewe haoni haja ya kwenda Mbwera kuona hali halisi ya kituo hicho baada ya kupokea taarifa kutoka kwa wataalamu wake kuona kama kimekamilika?
(b) Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha kwani wanaotakiwa ni 39 na sasa waliopo ni wanne tu?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Kituo cha Afya Mbwera kilifunguliwa muda mrefu na kinakabiliwa na uchakavu wa miundombinu na uhaba mkubwa wa watumishi ikiwemo madaktari, tabibu na wauguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo imepeleka jumla ya shilingi 560,000,000, kati ya fedha hizo shilingi 400,000,000 zimetolewa na Serikali kupitia wadau wa maendeleo wa Mfuko wa Afya wa Pamoja (Health Basket Funds) na shilingi 160,000,000, zimetolewa na Serikali ya Watu wa Korea kwa lengo la kuboresha miundombinu ikiwa ni pamoja na kujenga chumba cha upasuaji, nyumba ya mtumishi, wodi ya wazazi (maternity ward), jengo la maabara, kurekebisha mfumo wa maji safi na maji taka, chumba cha kuhifadhia maiti (mortuary) na kichomea taka (incinerator).
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa jengo la wodi ya wazazi na jengo la upasuaji yapo katika hatua ya msingi na ujenzi unaendelea kwa kutumia mfumo wa force account. Vilevile shilingi milioni 300 zimepelekwa bohari ya madawa (MSD) kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya Kituo cha Afya Mbwera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la watumishi wa afya Serikali inalitambua na mnamo mwezi Novemba, 2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti ilipewa watumishi wapya 11 wa kada mbalimbali za afya. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti imepanga kuajiri watumishi wapya wa kada mbalimbali za afya 199.