Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 27 Energy and Minerals Wizara ya Madini 224 2018-05-11

Name

Frank George Mwakajoka

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tunduma

Primary Question

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni kwa nini Serikali haiwapatii wananchi wa Mji wa Tunduma ruzuku ya asilimia 0.3 kama ilivyo kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye kuchimbwa madini?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 yaani Local Government Finance Act, Cap. 290, kifungu cha 6(1)(u), Halmashauri ulipo mgodi hutoza asilimia 0.3 ya mapato yote kabla ya kuondoa gharama za uzalishaji wa madini kama ushuru wa huduma yaani service levy. Aidha, kabla ya kuanza kutoza ushuru huo, Halmashauri husika inatakiwa kutunga Sheria Ndogo ya Halmashauri yaani District Council By-Laws ambazo zinaidhinishwa na Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa yaani TAMISEMI kwa mujibu wa kifungu cha 153(1) cha Mamlaka ya Serikali Mitaa yaani Local Government District Authority Act, Cap. 287.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, eneo la Halmashauri ya Tunduma hakuna leseni ya uchimbaji iliyotolewa. Hivyo, tunaendelea kuhimiza wawekezaji wa ndani na nje ili wawekeze katika utafiti na hatimaye kuanza kuchimba madini katika maeneo mbalimbali yenye madini nchini na Tunduma ikiwa mojawapo. Ahsante.