Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 27 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 225 2018-05-11

Name

Livingstone Joseph Lusinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtera

Primary Question

MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani juu ya wanyama waharibifu hususan tembo ambao wamesambaa hovyo katika Jimbo la Mtera na kufanya uharibifu mkubwa pamoja na kuua watu?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Jimbo la Mtera kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wanyamapori wakali na waharibifu limekuwa likijitokeza kwenye Wilaya zaidi ya 80 hapa nchini. Wanyamapori wakali na waharibifu ambao kwa kiwango kikubwa wamekuwa wakileta madhara kwa maisha ya binadamu na uharibifu wa mazao yao kisheria ni tembo, mamba, nyati, kiboko, simba, fisi na faru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la watu limesababisha kuzibwa kwa shoroba za wanyamapori pamoja na maeneo ya mazalia na mtawanyiko wao. Kuzibwa kwa shoroba hizo kumeongeza migogoro baina ya binadamu na wanyamapori. Hali hiyo kwa ujumla wake imeongeza ukubwa wa tatizo la mwingiliano kati ya binadamu na wanyamapori hususan tembo na hivyo kusababisha matukio mengi ya uharibifu wa mali na upotevu wa maisha ya binadamu katika maeneo mbalimbali likiwemo Jimbo la Mtera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali itaendelea kufanya doria za kudhiti wanyamapori katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Chamwino. Pia Wizara itaendelea kutoa elimu ya njia nyingine za kudhibiti tembo zikiwemo matumizi ya mizinga ya nyuki, uzio wa kamba uliopakwa mchanganyiko wa pilipili na oil chafu kuzunguka mashamba na kuchoma matofali ya kinyesi cha tembo kilichochanganywa na pilipili. Moshi unaotokana na uchomaji wa matofali ya kinyesi chenye pilipili ni mkali na hivyo hufukuza tembo mashambani kwa mafanikio makubwa. Njia hizi mbadala zimeonesha mafanikio makubwa pale zinapotumika vizuri na kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na mikakati hiyo, Serikali itaendelea kutoa fedha za kifuta jasho kwa uharibifu wa mali, yaani mazao na mifugo na kifuta machozi kwa wahanga waliouwawa au kujeruhiwa na wanyamapori hao. Kwa mfano, mwaka wa fedha 2017/2018 Wizara yangu imelipa jumla ya shilingi 7,520,000 kwa wananchi 27 wa Wilaya ya Chamwino walioathirika na wanyamapori.