Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 34 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 288 2018-05-22

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. EZEKIEL M. MAIGE (K.n.y. MHE. HUSSEIN N. AMAR) aliuliza:-
(a) Je, ni lini walimu wataboreshewa maslahi yao pamoja na nyumba za kuishi?
(b) Kwa juhudi za Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale ameweza kujenga madarasa mawili katika Kata ya Izunya kwa lengo la kuanzishwa shule ya sekondari tangu mwaka 2014. Je, ni kwa nini shule hiyo haijafunguliwa hadi sasa ili kuwapa moyo wafadhili?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Amar, Mbunge wa Nyang’hwale, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kuhakikisha walimu wa nchi hii wanaboreshewa maslahi yao ikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu. Katika kuboresha maslahi ya walimu, Serikali kwa Sheria Na. 25 ya mwaka 2015 ilianzisha Tume ya Utumishi ya Walimu ili iweze kusimamia na kushughulikia masuala yote yahusuyo maslahi ya walimu badala ya maslahi hayo kusimamiwa na chombo zaidi ya kimoja kama ilivyokuwa awali.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwezi Juni, 2015 hadi Desemba 2017, Serikali imetumia kiasi cha shilingi bilioni
33.135 kwa ajili ya kulipa madeni ya walimu ambapo walimu 86,234 wamelipwa nchi nzima. Aidha, katika kuhakikisha maslahi ya walimu yanayoboreshwa na kero zao zinaondolewa, jumla ya walimu 52 wa shule za msingi na sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale walilipwa jumla ya shilingi 99,685,990 za madai mbalimbali na wengine 202 walipandishwa vyeo (madaraja) katika mwaka wa fedha 2014/2015 na 2015/2016.
b) Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale, wananchi na uongozi wa Halmashauri ya Nyang’hwale kwa juhudi zao za kutaka kuiwezesha jamii kielimu wakiwemo wa Kata ya Izunya. Ili shule ya sekondari iweze kupewa kibali cha kufunguliwa wakati wa kuanzishwa inapaswa kwa kuanzia iwe na madarasa, kuwe na jengo la utawala, nyumba za walimu, vyoo vya walimu na wanafunzi, maktaba, viwanja vya michezo, samani pamoja na maabara kwa kuzingatia mwongozo uliowekwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa shule tarajiwa ya Izunya ina vyumba vya madarasa manne, vyoo matundu sita ya wasichana na wavulana matundu matano, jengo la utawala lenye vyoo vya walimu liko hatua za mwisho za umaliziaji na maabara zipo kwenye hatua ya jamvi. Hata hivyo, kwa kutambua jitihada za wadau mbalimbali wa elimu akiwepo Mheshimiwa Mbunge, Halmashauri imeazimia kutumia shilingi milioni 50 kutoka fedha za EP4R zilizopelekwa mwezi Februari, 2018 kwa ajili ya kukamilisha maabara zote. Ni matarajio yangu kwamba mara baada ya ujenzi wa maabara kukamilika taratibu za usajili wa shule hiyo zitakamilika. Aidha, naomba niitumie nafasi hii kutoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge, wadau wetu wa maendeleo na wananchi kwa ujumla kuunganisha nguvu zetu pamoja ili kukamilisha miundombinu inayohitajika katika shule kuweza kufunguliwa ikiwemo ya Kata ya Izunya.