Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 36 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 310 2018-05-24

Name

Dr. Ally Yusuf Suleiman

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mgogoni

Primary Question

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM (K.n.y. MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF aliuliza:-
Serikali iliunda Akaunti ya Pamoja ya Fedha kwa mujibu wa Ibara 133 ya Katiba kupitia Sheria Na.15 ya Mwaka 1984 ili kila upande usimamie uchumi wake na uchumi wa Muungano usimamiwe na chombo cha Muungano:-
• Je, ni kwa nini miaka 33 sasa Akaunti hiyo haijafanya kazi yake?
• Je, gharama kiasi gani imetumika kuanzisha taasisi ambayo haina faida yoyote?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Suleiman Ally Yussuf, Mbunge wa Magogoni, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua uwepo wa Akaunti ya Pamoja ya Fedha pamoja na Tume ya Pamoja ya Fedha. Ibara ya 133 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imebainisha sharti la kutungwa kwa sheria itakayoweka utaratibu wa uendeshaji wa Tume ya Pamoja ya Fedha pamoja na Akaunti ya Pamoja ya Fedha. Ili kutekeleza sharti hilo la kikatiba, Bunge lako Tukufu lilitunga Sheria ya Tume ya Pamoja ya Fedha ya Mwaka 1996 (The Joint Finance Commission Act, 1996) na hivyo kuwezesha kuanza kazi kwa Tume ya Pamoja ya Fedha mwaka 2003.
Mheshimiwa Spika, utaratibu wa uendeshaji wa Akaunti ya Pamoja ya Fedha umependekezwa kwenye ripoti ya mapendekezo ya vigezo vya kugawana mapato na kuchangia gharama za muungano iliyoandaliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha mwaka 2006. Hata hivyo, akaunti ya pamoja ya fedha haijaanza kufanya kazi kwa kuwa majadiliano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu mapendekezo ya Tume hayajakamilika.
(b) Mheshimiwa Spika, tangu kuzinduliwa kwake mwaka 2003 Tume ya Pamoja ya Fedha imekuwa ikiidhinishiwa bajeti yake na Bunge lako Tukufu kupitia bajeti ya Fungu 10, chini ya Wizara ya Fedha na Mipango. Katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2003/2004 hadi 2017/ 2018, Tume imeidhinishiwa bajeti ya Sh.31,971,490,663 kwa ajili ya uendeshaji na utekelezaji wa majukumu yake.
Mheshimiwa Spika, aidha, si kweli kwamba Tume ya Pamoja ya Fedha haina faida yoyote. Katika kutekeleza majukumu yake ya msingi, Tume imefanya stadi sita tangu kuanzishwa kwake kwa lengo la kutoa mapendekezo na ushauri katika eneo la uhusiano wa kifedha kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Pia, Tume ya Pamoja ya Fedha imeandaa rasimu ya Mwongozo wa Uendeshaji wa Akaunti ya Fedha ya Pamoja ambao unatarajiwa kutekelezwa mara majadiliano ya pande mbili za Muungano yatakapokamilika.