Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 21 2018-09-05

Name

Susan Limbweni Kiwanga

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Mlimba

Primary Question

MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Serikali iliahidi kuweka mipaka ya kutenganisha Vijiji vya Jimbo la Mlimba na RAMSAR SITE kwa kuwashirikisha wanavijiji wa maeneo husika lakini kazi hiyo haikufanyika badala yake wakulima waliambiwa mwisho wao kwenye maeneo hayo ni mwezi Agosti na wafugaji mwisho wao kwenye maeneo yao ni Julai:-
• Je, kwa nini Serikali haikutekeleza jukumu lake la kuweka mipaka badala yake wakulima na wafugaji wamepewa barua ya kusitisha kutumia maeneo hayo na kusababisha taharuki kubwa kwa wananchi?
• Kwa kuwa wananchi hao walifungua kesi kupinga maonevu hayo mwaka 2015 kesi Na. 161 kuhusu mgogoro huo na bado kesi hiyo haijakwisha, kwa nini Serikali imewasitisha wananchi hao kuendelea kutumia maeneo hayo kabla ya kesi haijakamilika?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekaji wa alama za mipaka kwenye maeneo yaliyohifadhiwa kisheria hufanyika kwa kuwashirikisha wananchi wa maeneo husika. Katika Pori Tengefu la Kilombero, zoezi la uwekaji wa alama za mipaka (vigingi) limefanyika kwa kuwashirikisha wananchi ambapo hadi kufikia Agosti, 2018, jumla ya vigingi 143 vimesimikwa kwa upande wa Wilaya za Malinyi na Ulanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika Wilaya ya Kilombero zoezi la uelimishaji wananchi limefanyika katika vijiji saba vya Miwangani, Namwawala, Idandu, Mofu, Ikwambi, Miomboni na Kalenga. Baada ya hatua hiyo, uwekaji wa alama ya mipaka utaendelea na utashirikisha wananchi wa maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wananchi walifungua Kesi ya Ardhi Na.161 ya mwaka 2015 kupinga zoezi la Operesheni Okoa Bonde la Kilombero iliyofanyika mwaka 2012 kwa madai ya kuwa watu wanaofanya shughuli katika bonde hilo walipwe stahiki zao na kupewa muda muafaka wa kuondoka. Hoja ya wananchi hao ililenga kuiomba Mahakama izuie Serikali katika kuendesha operesheni tajwa kupitia Shauri Na.357 la Mwaka 2017 yaani Miscellaneous Land Application No.357 of 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Mahakama kusikiliza ombi la wananchi hao ilionekana kutokuwa na tija hivyo ikaamua kutokukubaliana na shauri hilo na badala yake ikaelekeza kesi ya msingi Na. 161 ya mwaka 2015 iendelee kusikilizwa, kesi hiyo itatajwa tena tarehe 19/9/2018. Hata hivyo, kesi iliyopo mahakamani kwa sasa haizuii Serikali kuendelea na operesheni itakayosaidia kuokoa Bonde la Kilombero ambalo ni muhimu sana katika kulinda ardhi oevu na ni chanzo kikubwa cha maji ya Mto Rufiji unaotegemewa kwa uzalishaji wa umeme kupitia mradi wa Rufiji.