Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 2 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 22 2018-09-05

Name

Athumani Almas Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Kaskazini

Primary Question

MHE. ALMAS A. MAIGE aliuliza:-
Hivi karibuni Serikali kupitia JKT imeanzisha tena mafunzo ya vijana wa kujitolea na wale wa mujibu wa sheria waliomaliza kidato cha sita au kutoka vyuo hapa nchini.
• Je, ni kweli kuwa JKT wanachukua wanafunzi kwa mujibu wa sheria kutoka katika shule na vyuo vya Serikali tu?
• Je, Serikali haioni kuwa vijana kutoka shule na vyuo binafsi wanahitaji pia mafunzo muhimu ya uzalendo na kujiendeleza kiuchumi?
• Je, ni vijana wangapi kwa mujibu wa sheria kwa mwaka 2017/2018 wamechukuliwa na JKT katika shule na vyuo binafsi nchini?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wa mujibu wa sheria huchukuliwa moja moja kutoka shule za Serikali na binafsi bila kuhusisha vyuo. Vijana kutoka vyuo vya Serikali na binafsi hujiunga na mafunzo ya JKT kwa utaratibu wa kujitolea ambapo utaratibu wa kuwapata hupitia katika usaili unaofanyika ngazi za Wilaya na Mikoa ambapo unahusisha pia vijana wengine wenye sifa bila kujali shule aliyotoka.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaona umuhimu wa kuchukua vijana kutoka shule na vyuo binafsi kwa ajili ya mafunzo katika Jeshi la Kujenga Taifa, ndiyo maana uteuzi wa vijana unahusisha shule zote za Serikali na binafsi. Vijana ambao ni wahitimu wa vyuo vya Serikali au binafsi huingia JKT kwa utaratibu wa kujitolea kama nilivyosema awali.
c) Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana waliojiunga na JKT kutoka shule binafsi idadi yao ni 7,076 ambapo kati yao wavulana ni 5,432 na wasichana ni 1,644. Idadi hiyo ni kati ya vijana 20,000 walioitwa kujiunga na mafunzo kwa mujibu wa sheria kwa mwaka 2017/2018.