Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 4 Energy and Minerals Wizara ya Madini 52 2018-09-07

Name

Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Primary Question

MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-
Wilaya ya Ileje imejaliwa kuwa na rasilimali ya makaa ya mawe ya Kiwira na Kabulo na STAMICO imekaririwa kuanza rasmi kuuza makaa hayo kwa kasi ili kukidhi mahitaji ya viwanda vya saruji na kukuza pato la Taifa, aidha, STAMICO ilianza uzalishaji wa majaribio ya makaa ya mawe katika Mgodi wa Kabulo tarehe 30/04/2017.
(a) Je, Mgodi wa Kabulo utaendelea kuchimba baada ya majaribio hayo na ni nani anayefanya uchimbaji huo?
(b) Je, kuna makubaliano gani na Wilaya ya Ileje juu ya mrahaba na uchumi kwa wana Ileje?
(c) Je, ni lini Mgodi wa Kiwira utaanza kufanya kazi na ni nini hasa kinachokwamisha?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la mama yangu, Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Jimbo la Ileje, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) lilianzishwa mwaka 1972 likiwa na jukumu la kushiriki na kusimamia maslahi ya Serikali katika sekta ya madini pamoja na rasilimali ya madini. Aidha, mwaka 2005 Mgodi wa Kiwira ulibinafsishwa kwa kampuni binafsi ya wazawa ya Tan Power Resources Ltd. (TPR) kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa umeme na kufikia megawati 200. Mnamo tarehe 30, Juni, 2014 Serikali iliikabidhi STAMICO Mgodi wa Kiwira kutokana na mbia mwenza kukosa mtaji wa kuendesha mgodi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, STAMICO ilianza uchimbaji wa majaribio katika leseni yake ya makaa ya mawe ya Kabulo mnamo mwezi Aprili, 2017 ambapo katika kazi hiyo jumla ya tani 8,674 za makaa ya mawe zilichimbwa. Baada ya kukamilisha majaribio ya awali STAMICO imeanza mchakato wa kumpata mkandarasi atakayefanya uchimbaji. Lengo ni mkandarasi huyo aanze kazi ya uchimbaji utakaozingatia taratibu zote za uchimbaji, mazingira na usalama mgodini katikati ya mwaka huu wa fedha yani 2018/ 2019.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, STAMICO kama ilivyo kwa wamiliki wengine wenye leseni za uchimbaji wa madini inawajibika kulipa ushuru wa huduma kwa Halmashauri wa asilimia 0.3 ya mapato ghafi yatokanayo na mauzo ya makaa ya mawe. STAMICO tayari imeanza kulipa ushuru wa huduma kwa Halmashauri ya Wilaya hiyo kutokana na mauzo ya makaa yaliyofanyika ambapo kiasi cha shilingi 57,600 kimelipwa. Aidha, jumla ya shilingi 1,735,900 zimelipwa kama ushuru wa barabara kwa Halmashauri. Manufaa mengine ni pamoja na kutoa ajira kwa wananchi wa Wilaya ya Ileje na kuchangia huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo afya, elimu na maji.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, STAMICO ilikabidhiwa Mgodi wa Kiwira mnamo mwezi Juni, 2014 ili kuendesha na kuusimamia kufuatia Kampuni ya Tan Power Resources kuurejesha Serikalini. Aidha, STAMICO imeendelea na jitihada mbalimbali za kutafuta fedha ikiwa ni pamoja na kutafuta wabia wenye uwezo watakaoshirikiana na shirika katika uendeshaji wa mradi huu.