Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 5 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 56 2018-09-10

Name

Mussa Bakari Mbarouk

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Tanga Mjini

Primary Question

MHE. MUSSA B. MBAROUK aliuliza:-
Kumekuwa na sintofahamu kwa baadhi ya wafanyabiashara na TRA kuhusu mashine za EFDs hususani bei za mashine na aina za mashine.
(a) Je, bei halali ya mashine ya EFD kulingana na aina na ubora wake ni shilingi ngapi?
(b) Kwa kuwa mashine za EFDs zinafanya kazi kwa niaba ya TRA, je, kwa nini Serikali isitoe mashine hizo bure kwa wafanyabiashara?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Spika, kuna aina tano za mashine za EFD kwa ajili ya kutunza kumbukumbu na kutoa risiti za mauzo. Mfanyabiashara anaweza kununua aina mojawapo ya mashine hizo kulingana na mahitaji yake. Aidha, ubora wa mashine zote ni lazima uthibitishwe na Mamlaka ya Mapato Tanzania kabla mashine hizo hazijaingia sokoni na kuanza kutumika. Bei ya kila mashine ni kama ifuatavyo:-
i. Rejista za Kielekroniki za Kodi - mashine hizi hutumiwa na wafanyabiashara wasiotumia mifumo ya kompyuta au mifumo ya kihasibu na bei yake kwa sasa ni shilingi 590,000.
ii. Mashine za kielektroniki zinazoweka alama au saini (Electronic Signature Devices) - mashine hizi hutumiwa na walipakodi wanaotumia mifumo ya kompyuta na mifumo maalum ya kihasibu na bei zake ni kati ya shilingi 1,000,000 na 1,200,000.
iii. Printa za Kielektroniki za Kodi (Electronic Fiscal Printers) - mashine hizi hutumia mfumo maalum wa kompyuta kufanya mauzo na bei zake ni kati ya shilingi 1,500,000 na 1,700,000.
iv. Printa za Pampu za Mafuta ya Petroli na Dizeli - mashine hizi hutumiwa na wafanyabiashara wanaouza mafuta ya petroli na dizeli kwa kutumia pampu na bei zake ni shilingi 6,000,000 ikijumuisha gharama za ufungaji na uunganishaji kwenye pampu za mafuta.
v. Printa za Maduka ya Kubadilisha Fedha za Kigeni - bei za mashine hizi ni shilingi 2,150,000 ikiwa ni pamoja na programu ya mfumo (software).
b) Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara wanaponunua mashine za EFD hulipa gharama za ununuzi wa mashine hizo na baadaye Serikali hurejesha gharama hizo kama ifuatavyo:-
i. Wafanyabiashara waliosajiliwa kwenye VAT; kwa mujibu wa jedwali la saba chini ya Kanuni ya 54(2) za Sheria ya Usimamizi wa Kodi za mwaka 2016, mashine zilizonunuliwa kwa mara ya kwanza zinagharamiwa na Serikali kwa kumruhusu mfanyabiashara kujirejeshea fedha zake kwa utaratibu wa input – output tax kwenye return yake ya mauzo ya mwezi husika.
ii. Kwa wafanyabiashara ambao hawajasajiliwa kutoza Kodi ya Ongezeko la Thamani hurejeshewa gharama za mashine kama ifuatavyo:-
Mosi, wanaoandaa hesabu za mizania; kundi hili linaruhusiwa kujirejeshea gharama za ununuzi wa mashine kwa kuziingiza gharama husika kama gharama za kuendesha biashara kama ilivyoainishwa kwenye kifungu cha 11(2) cha Sheria ya Kodi ya Mapato.
Pili, wafanyabiashara wasioandaa hesabu za mizania (presumptive cases) kwa mujibu wa Kanuni ya 54(2) ya Kanuni za Sheria ya Usimamizi wa Kodi za mwaka 2016 kundi hili la wafanyabiashara wanajirejeshea gharama za mashine kwenye kiasi cha kodi walichokadiriwa kwa mwaka husika. Kama hawatakuwa wamejirejeshea kwa asilimia 100 basi kiasi kilichobakia kitasogezwa mwaka unaofuata.