Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 8 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 103 2018-09-13

Name

Ester Alexander Mahawe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER M. MMASI (K.n.y. MHE. ESTER A. MAHAWE) aliuliza:-
Gharama za kupanda Mlima Kilimanjaro ni mara mbili ya gharama za kupanda Mlima Kenya; hali hii imesababisha kushuka kwa idadi ya watalii na kuinyima Serikali mapato. Je, ni lini Serikali itafanya marekebisho ya bei hizo?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mlima Kilimanjaro ni mlima mrefu kuliko yote Barani Afrika ukiwa na urefu wa mita 5,895 kutoka usawa wa bahari. Mlima huu una sifa nyingi za kipekee ikiwemo ya kuwa mlima mrefu duniani uliosimama peke yake (the only free standing mountain in the world), asilimia 85 ikiwa ni vertical, wenye barafu japo upo katika Ukanda wa Ikweta. Ni moja ya eneo la Urithi wa Dunia na umetunukiwa tuzo ya kuwa kivutio bora (One of the Africa Wonders).
Mheshimiwa Spika, aidha, Mlima Kilimanjaro una aina zaidi ya 200 ya ndege na zaidi ya aina species 140 za mamalia wakiwemo tembo, pofu, pongo, jamii ya swala, minde, twiga, simba, chui na wengineo, sifa ambazo Mlima Kenya hauna.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kununi za kupanda mlima, Mlima Kilimanjaro hupandwa kwa wastani wa siku sita. Safari ya kupanda mlima huu kwa mtalii kutoka nje ya nchi huipatia Serikali mapato ya dola za Kimarekani 684.4 pamoja na kodi ya VAT. Mtalii anayepanda Mlima Kenya kwa siku sita hulipa dola za Marekani 460. Tofauti ya gharama kati ya milima hii zinatokana na umuhimu wa kipekee pamoja na sifa ya Mlima Kilimanjaro ambazo haziwezi kulinganishwa na Mlima Kenya.
Mheshimiwa Spika, njia ya kupanda Mlima Kilimanjaro zimetengenezwa vizuri kiasi cha kuwezesha mtu wa kawaida asiye na utaalam kupanda mlima hadi kileleni wakati kwa Mlima Kenya upandaji unahitaji utalaam (technical climbing). Tofauti hizi husababisha gharama za utalii kati ya milima hii zisifanane.
Mheshimiwa Spika, mwaka 2017/2018 Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro ilipokea na kuhudumia watalii 51,825 ambao waliingizia Taifa mapato ya shilingi bilioni 76.16. Kwa sasa Serikali imepanga kukutana na wadau wa Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro ili kukubaliana masuala mbalimbali ikiwemo bei ya kupanda Mlima Kilimanjaro.