Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 44 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 377 2018-06-05

Name

Dr. Haji Hussein Mponda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Malinyi

Primary Question

MHE. HADJI H. MPONDA aliuliza:-
Serikali kupitia aliyekuwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Pinda alitoa agizo la kuweka utatuzi wa kudumu katika migogoro ya ardhi iliyopo baina ya wananchi na Serikali katika maeneo ya vijiji na mapori tengefu. Aidha, katika kampeni zake Wilayani Malinyi Mheshimiwa Rais aliahidi uhaulishwaji wa Buffer Zone ya pPori Tengefu la Kilombero kwa vijiji vinavyopakana ili wawe huru katika shughuli zao, lakini hadi leo hakuna utekelezaji wowote.
(a) Je, utekelezaji wa ahadi na agizo hili umefikia wapi?
(b) Je, Serikali ina mpango mbadala kwa wananchi wanaoishi kihalali katika maeneo hayo ya Buffer Zone ya Pori Tengefu la Kilombero?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda Mbunge wa Malinyi lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianza kutekeleza agizo la Mheshimiwa Waziri Mkuu mstaafu mwezi Februari, 2016 wakati ilipozindua programu maalum ya upimaji wa vijiji na urasimishaji wa ardhi (Land Tenure Support Programme) vya Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi unaosimamiwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Programu hiyo ya miaka mitatu inafadhiliwa na DFID, DANIDA na SIDA kwa jumla ya dola za Kimarekani milioni 15.2.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwezi Mei, 2018 jumla ya vijiji 12 kati ya vijiji 14 vinavyopakana na hifadhi katika Wilaya ya Malinyi vimepimwa. Hii ni sawa na asilimia 85.71 ya vijiji vinavyotarajiwa kupimwa. Aidha, katika Wilaya ya Ulanga jumla ya vijiji saba vimepimwa na kati ya hivyo vijiji vitano alama za mipaka zimeshawekwa. Katika Wilaya ya Kilombero jumla ya vijiji 22 vinavyopakana na hifadhi vinatarajiwa kupimwa. Elimu na uhamasishaji umefanyika katika vijiji saba vya Wilaya hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mpango huu, Serikali inaamini kwamba matumizi ya ardhi katika maeneo yanayozunguka Pori Tengefu la Kilimanjaro yakiwemo maeneo ya Wilaya ya Malinyi yatawekwa bayana na hivyo kupatikana kwa utatuzi wa kudumu wa migogoro ya ardhi iliyopo baina ya wananchi na Pori Tengefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizo, Serikali imeunda Kamati Maalum kwa ajili ya kuongea na wadau mbalimbali kwa lengo la kupata picha halisi ya mgogoro ili kutoa ushauri na mapendekezo yatakayowezesha kupata suluhu ya kudumu ya mgogoro wa matumizi ya ardhi katika Bonde la Kilombero. (Makofi)