Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 47 Public Service Management Ofisi ya Rais TAMISEMI. 398 2018-06-08

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Utumishi wa umma ndiyo injini ya maendeleo katika nchi. Watumishi wa umma hawatakiwi kuwa na mrengo wowote wa itikadi ya kisiasa ili kutumikia wananchi kwa muda wote hata yanapotokea mabadiliko ya vyama tawala baada ya uchaguzi.
i. Je, Serikali ya Awamu ya Tano ina mkakati gani wa kuhakikisha utumishi wa umma ni thabiti na wa kuaminika wakati wote?
ii. Je, ni watumishi wangapi wa umma ambao wamegombea vyeo katika chama tawala wakati wapo katika ajira ya utumishi wa umma?

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Katibu Mkuu Mstaafu, senior citizen mwenzangu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ya 65(1), Jedwali la Tatu, Sehemu ya IX ya Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003 ikisomwa kwa pamoja na aya ya 50 ya Taratibu za Uendeshaji Utumishi wa Umma za mwaka 2003, watumishi wa umma wanatakiwa kutokuwa na mrengo wowote wa itikadi ya siasa ili kuwatumikia wananchi kwa muda wote bila ubaguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulihakikishia Bunge lako tukufu kuwa kanuni hizi zimeendelea kuwepo pia katika Serikali ya Awamu ya Tano na hivyo kuendelea kuimarisha utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Na.1 wa mwaka 2015 unaosimamia ushiriki wa watumishi wa umma katika uongozi wa kisiasa watumishi wote wa umma waliogombea na kupata nafasi za uongozi wa kisiasa walistaafu na hawapo tena katika utumishi wa umma.