Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 48 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 406 2018-06-11

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. ALHAJ A. BULEMBO (K.n.y MHE. HUSSEIN N. AMAR) aliuliza:-
Taasisi za umma na taasisi binafsi zimeitikia wito wa Mheshimiwa Rais wa kutengeneza madawati kwa ajili ya shule zetu nchini:-
Je, Serikali na mamlaka husika zimejipanga vipi katika kuhakikisha utunzaji bora wa madawati hayo?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang’wale, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inazipongeza na kuzishukuru taasisi zote za umma na za binafsi zilizoitikia wito wa Serikali wa kutengeneza madawati ya kutosha kwa ajili ya shule zetu nchini. Katika kuhakikisha kuwa madawati yaliyotengenezwa kwa ajili ya shule za msingi na sekondari yanatunzwa vizuri na yanadumu kwa muda mrefu, Serikali kupitia Mwongozo wa Matumizi ya Fedha za Ruzuku ya Uendeshaji (Capitation Grants) wa tarehe 28 Desemba, 2015 imeelekeza kuwa asilimia 30 ya fedha hizo itumike kwa ajili ya ukarabati wa samani ikiwemo madawati kwa upande wa shule za msingi na asilimia 10 kwa upande wa shule za sekondari.
Mheshimiwa Spika, aidha, Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa na shule zote wameelekezwa kutotumia madawati hayo kwa shughuli nyingine, kwa mfano, mikutano ya kijiji, vyama vya siasa na matumizi mengine yasiyokusudiwa ili kupunguza kasi ya uharibifu. Ukaguzi wa mara kwa mara umeagizwa kufanyika kwa kushtukiza ili kuhakikisha madawati yaliyopo yanatunzwa vyema.