Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 52 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 439 2018-06-18

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Serikali imetumia zaidi ya shilingi milioni 350 kuimarisha barabara ya Namanyere – Ninde yenye urefu wa kilomita 67, lakini fedha hazikutosha kukamilisha barabara hiyo:-
Je, Serikali itatenga fedha zaidi kukamilisha barabara hiyo?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Barabara ya Namanyere- Ninde yenye urefu wa kilomita 67, kwa mara ya kwanza iliibuliwa na mradi wa TASAF Awamu ya I mwaka 2005/2006 kwa kulima barabara hiyo kwa kutumia nguvu kazi ya wananchi. Kwa kipindi chote hadi mwaka 2014/2015, barabara haikufunguka kwa kukosa miundombinu muhimu kama vile madaraja na makalvati.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015, Serikali ilitenga fedha jumla ya shilingi milioni 375.3 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo ambapo fedha hizo zilitumika kwa kufyeka barabara na kuondoa miti katika barabara yote, kuilima barabara kwa urefu wa kilomita 25 kwa kiwango cha udongo, kujenga Makalvati 15 pamoja na kujenga madaraja manne. Kati ya madaraja manne yaliyojengwa, mawili yapo katika Mito ya Lwafi na Ninde, hivyo matengenezo hayo yamewezesha barabara hiyo kufunguka kwa urefu wa kilomita 25 tu.
Mheshimiwa Spika, kulingana na upatikanaji wa fedha, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kufanyia matengenezo barabara hiyo ambapo mwaka wa fedha 2015/2016, shilingi milioni 44.58 zilitengwa kwa ajili ya kufanya matengenezo ya muda maalum kwa urefu wa kilomita 20. Aidha, mwaka wa fedha 2016/2017, kiasi cha shilingi milioni 20 zilitumika kuimarisha sehemu korofi zenye urefu wa mita 500.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuifungua barabara hii kadri fedha zitakavyokuwa zinapatikana ili kusaidia wananchi wanaotumia barabara hii katika suala zima la usafiri.