Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 53 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 447 2018-06-19

Name

Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. SAED A. KUBENEA) aliuliza:-
Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alipotembelea Kituo cha Afya cha Palestina kilichopo Kata ya Sinza alitangaza kukipandisha hadhi kuwa Hospitali ya Wilaya. Hata hivyo, bado Serikali inaendelea kuipatia fedha hospitali hiyo kama Kituo cha Afya.
Je, ni lini Serikali itaitambua hospitali hiyo kama Hospitali ya Wilaya kwa kuipa fedha na vitendea kazi vinavyofanana na hadhi yake?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Ubungo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Palestina kimekuwa kinafanya kazi kama Hospitali ya Wilaya kufuatia tamko la Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne la tarehe 11 Disemba, 2012.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya tamko hilo, ukaguzi ulifanyika na kubaini uhitaji wa kuongezewa eneo kwa ajili ya upanuzi wa huduma. Ifahamike wazi kuwa kituo hiki kilianzishwa ili kitoe huduma kama Kituo cha Afya, hivyo hakiwezi kuwa Hospitali ya Wilaya. Kwa kutambua umuhimu wa kituo hiki, hatua zifuatazo zimechukuliwa kutatua baadhi ya changamoto:-
(a) Kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ruzuku ya ununuzi wa dawa, vifaatiba na vitendanishi kutoka Bohari Kuu ya Dawa (MSD) imeongezeka hadi kufikia shilingi milioni 69 kutoka shilingi milioni 57.4 kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
(b) Madaktari Bingwa watatu wameshapelekwa katika kituo hiki kati ya watano wanaohitajika, kwa maana ya Madaktari Bingwa wa Watoto, wawili na Daktari wa Magonjwa ya Wanawake na Uzazi mmoja.
(c) Katika mwaka wa fedha 2018/2019, kiasi cha shilingi milioni 160 kimetengwa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo la ghorofa moja ambalo lina wodi ya wanaume, wanawake na watoto.
(d) Kwa mwaka wa fedha 2018/2019 kituo kimetengewa asilimia 25 ya fedha za Mfuko wa Pamoja wa Wafadhili (Health Sector Basket Fund) ambayo ni sawa na shilingi milioni 357.73 ya mgao wa Manispaa ya Ubungo ambayo ni shilingi bilioni 1.43. Fedha hizi ni kwa ajili ya utawala na ununuzi wa dawa na vifaa tiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako tukufu, napenda kuelekeza Halmashauri ya Ubungo kutenga eneo lisilopungua ekari 25 litakalowezesha kuwepo katika eneo moja majengo yote ya msingi ya Hospitali ya Wilaya. Aidha, Serikali itaendelea kupeleka Madaktari Bingwa na kuboresha huduma zaidi katika kituo hiki kadri bajeti itakavyokuwa ikiruhusu.