Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 57 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 484 2018-06-25

Name

Dr. Pudenciana Wilfred Kikwembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kavuu

Primary Question

MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE aliuliza:-
Katika Bunge lililopita la 2010 – 2015 Serikali iliongelea kuhusu mpango wa kuwekeza umeme unaotumia chemchemi ya maji ya moto yanayopatikana katika Kata ta Maji Moto:-
a) Je, mpango huo umefikia wapi?
b) Je, ni lini sasa Jimbo la Kavuu litapata umeme kwa maendeleo ya wananchi wa eneo hilo?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pudenciana Wilfred Kikwembe, Mbunge wa Kavuu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Katavi ni moja ya mikoa inayopitiwa na Bonde la Ufa la Afrika Mashariki, hivyo kuwepo na uwezekano wa kuwa na hifadhi kubwa ya joto ardhi. Serikali inaendelea kufanya tathmini ya rasilimali ya nishati ya joto ardhi ili kujiridhisha na uwepo wa rasilimali ya kutosha kabla ya kuchoronga visima vya majaribio. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali kupitia Tanzania Geothermal Development Company imepanga kufanya utafiti wa kina katika maeneo zaidi ya 50 yenye viashiria vya joto ardhi likiwemo eneo la Maji Moto.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Jimbo la Kavuu vya Kibaoni, Usevya, Ilalangulu na Manga, vinapata umeme kutoka Sumbawanga, Mkoani Rukwa kupitia Mji wa Namanyere, Wilayani Nkasi. Aidha, vijiji vingine vya Jimbo la Kavuu ikiwa ni pamoja na Maji Moto, Mbende, Chamalangi, Mkwajuni, Ikuba, Mamba na Kasansa vitapatiwa umeme kupitia mzunguko wa kwanza wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupatikana kwa suluhisho la kudumu la umeme katika Jimbo la Kavuu, Serikali imeanza hatua za awali za utekelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa gridi, kV 400 kutoka Mbeya – Sumbawanga – Mpanda – Kigoma hadi Nyakanazi. Ujenzi wa mradi huu unatarajiwa kuanza Machi, 2019 na kukamilika mwaka 2021. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)