Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 60 Energy and Minerals Wizara ya Madini 507 2018-06-28

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-
Wawekezaji wanaotaka kuja kuwekeza kwenye Sekta ya Nishati na Madini wamepungua sana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita:-
(a) Je, ni nini kimesababisha hali hiyo?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha kuwa Wawekezaji wanaendelea kuja ili kukuza uwekezaji kutoka nje (Foreign Direct Investment] (FDI)?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, vichocheo vikuu vitatu vya uwekezaji katika Sekta ya Madini katika nchi yoyote, cha kwanza ni jiolojia inayoashiria uwezekano wa uwepo wa madini (prospective geology). Pili ni mwenendo wa bei ya madini husika kwenye Soko la Dunia na tatu Sera za Uchumi Mkuu (Macroeconomics) za nchi husika. Ilani ya CCM tunayoitekeleza hivi sasa ilizingatia vigezo hivi kwa kuhimiza kujenga uwezo wa Geological Survey of Tanzania ili waweze kugundua mashapo ya madini, kupunguza gharama za uzalishaji kwa kuboresha miundombinu na kuongeza thamani ya madini ili yawe na bei nzuri kwenye soko la dunia na kubadili Sheria ya Madini ili kuongeza uwazi na manufaa kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha miaka mitano nchi yetu imeendelea kupokea wawekezaji kwenye sekta ya madini. Jumla ya leseni 102 za uchimbaji mkubwa (Special Mining Lenience) na wa kati (Mining License) zimetoelewa kati ya mwaka 2012/2013 hadi 2016/2017, ikiwa ni wastani wa leseni 20 kwa mwaka. Aidha, mwaka wa fedha 2012/2013 hadi 2016/2017 leseni 3,136 za utafutaji wa Madini (Prospecting License) zilitolewa, hii ikiwa ni wastani wa leseni 627 kwa mwaka. Mwaka 2017/2018, tumepokea maombi 26 ya Special Mining License na Mining License, yaani uchimbaji wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepokea maombi 818 ya leseni za utafiti wa madini (Prospecting License). Tume ya Madini iliyoundwa hivi karibuni inaendelea kupitia maombi hayo na iwapo yatabainika kukidhi vigezo vya kisheria leseni hizi zitatolewa na hivyo kuendelea kuchangia kuongezeka kwa Foreign Direct Investment (FDI). Kwa takwimu hizi, bado wawekezaji wanaonesha nia ya dhati kuwekeza nchini kwani nchi yetu inakidhi sifa tatu nilizoainisha hapo awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuchukua hatua za makusudi kuandaa mazingira rafiki ya kuvutia wawekezaji na kutangaza fursa zilizopo nchini. Hatua zinazochukuliwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu wezeshi kama vile ujenzi wa barabara, reli, kupanua bandari, kujenga miundombinu, maji, umeme, gesi na mawasiliano kuelekea maeneo yanayotazamiwa kuanzishwa migodi. Aidha, Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) kwa kuwapatia wataalam vitendea kazi ili kuwawezesha kuongeza kasi ya kufanya tafiti za kina za maeneo yenye madini nchini. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.