Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 68 2018-04-13

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Serikali kupitia Mradi wa Mfuko wa Benjamin Mkapa ilidhamiria kujenga na kukamilisha huduma ya upasuaji kwenye Kituo cha Afya cha Kata ya Kala na baada ya mfuko huo kuacha shughuli zake hakuna juhudi inayoendelea.
(a) Je, kuna mpango wowote kuendeleza nia hiyo njema?
(b) Kwa kuwa kituo hicho kina upungufu mkubwa wa wataalam; je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi wakiwepo wauguzi?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa za Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ina vituo vya afya saba, kati ya hivyo vituo vinne vinamilikiwa na taasisi za kidini na vitu vitatu vinamilikiwa na Serikali. Vituo vya afya viwili vinavyomilikiwa na Serikali vinatoa huduma za upasuaji. Kituo cha Afya Kala kinamilikiwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Sumbawanga. Taasisi ya Benjamin Mkapa ilijenga chumba cha upasuaji (theatre) pamoja na kutoa baadhi ya vifaa kwa ajili ya huduma za upasuaji katika Kituo cha Afya Kala mnamo mwaka 2016/2017.
Hata hivyo, huduma hizo zimekuwa hazitolewi kutokana na changamoto mbalimbali kubwa zikiwa ni upatikanaji wa wataalam kwa ajili ya kufanya huduma za upasuaji na kukosekana kwa huduma ya umeme na mfumo wa maji kwa ajili ya kuendeshea shughuli za upasuaji. Ili kukabiliana na hali hiyo Halmashauri imetenga kiasi cha shilingi milioni 17.3 katika mwaka wa fedha 2017/2018, kwa ajili ya miundombinu ya maji na umeme ambapo fedha hiyo bado haijapokelewa.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na upungufu wa watumishi katika Kituo cha Afya Kala, Halmashauri ilipeleka tabibu mmoja na wauguzi wawili ili kutoa huduma katika kituo hicho mwaka 2015. Aidha, Halmashauri ilipeleka gari moja la wagonjwa lenye namba za usajili SM 4467 mwaka 2017 kutoa huduma katika kituo hicho. Serikali itaendelea kupeleka wataalam wa afya katika kituo hicho kwa kadri watakavyopatikana. Serikali inaendelea kufanya mazungumzo na wamiliki wa Kituo cha Afya Kala ili kushirikiana katika kutatua changamoto ya watumishi katika kituo hicho kwa kuwa watumishi watatu waliopo sasa katika kituo hicho wote wameajiriwa na Serikali.