Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 9 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 72 2018-04-13

Name

Albert Ntabaliba Obama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Primary Question

MHE. ALBERT O. NTABALIBA aliuliza:-
Utekelezaji wa mradi wa umeme wa REA Wilayani Buhigwe unasuasua sana.
Je, ni lini vijiji vyote na vitongoji vyake pamoja na taasisi za umma zitapata umeme?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Albert Obama Ntabaliba, Mbunge wa Buhigwe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Buhigwe ina kata 20, vijiji 44 na vitongoji 190. Kupitia Miradi ya REA Awamu ya Pili vijiji 14 vilipatiwa umeme, vijiji hivyo ni Kasumo, Kalege, Nyanga, Biharu, Kigege, Bulimanyi, Nyamugali, Songambele, Kavomo, Buhigwe, Mulera, Munanila, Manyovu na Mwayaya. Aidha, katika awamu hiyo taasisi mbalimbali za umma zilipatiwa umeme ikiwamo Shule ya Msingi ya Kalege, Kituo cha Afya cha Muyama, Zahanati ya Buhigwe, Kituo cha Polisi cha Buhigwe, pamoja na Ofisi ya Uhamiaji ya Munanila nayo ilipatiwa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vipatavyo 22 vya Wilaya ya Buhigwe vimejumuishwa katika Mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza unaotarajiwa kuanza kutekelezwa Mwezi Mei, 2018 katika Wilaya za Buhigwe, Kasulu, Kigoma na Uvinza. Utekelezaji wa mradi huu umechelewa kuanza katika Wilaya hizo kutokana na mmoja wa wakandarasi walioomba kazi hiyo kuilalamikia kampuni iliyokusudiwa kupewa kazi hiyo mahakamani. Vijiji vitakavyopelekewa umeme ni pamoja na Nyakimwe, Mkatanga, Rusaba, Nyaruboza, Muhinda, Kibande, Kajana, Bweranka, Kigogwe, Kibwigwa, Kinazi, Kitambuka, Munzese, Bukuba, Nyankoronko, Migongo, Mubanga, Mugera, Kirungu, Katundu, Munyegera na Nsagara. Kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilometa 103.64 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 na kilometa 142 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 71 na uunganishwaji wa wateja wa awali 3,011. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 8.53.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vyote na vitongoji vyake pamoja na taasisi za umma zitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu baada ya taratibu zote zinazoendelea kukamilika. Vijiji nane vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia awamu ya tatu mzunguko wa pili ambao unatarajiwa kuanza Novemba, 2019 na kukamilika Juni, 2021, ahsante.