Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 24 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 199 2018-05-08

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali italeta mabadiliko katika sheria inayosimamia malipo ya fidia kwa askari anayejeruhiwa au kupoteza maisha akiwa anatekeleza majukumu ya kulinda usalama ndani au nje ya nchi kwenye vyombo vya UN au SADC Mission ili kuendana na mabadiliko ya kupanda kwa gharama za maisha?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, malipo ya fidia kwa askari aliyejeruhiwa au kufariki akiwa anatekeleza majukumu ya ulinzi wa amani katika Umoja wa Mataifa hupangwa na kusimamiwa na Umoja wa Mataifa. Kwa kawaida, Umoja wa Mataifa hukaa vikao vya maamuzi na kutoa waraka ambao kwa ujumla hutekelezwa na nchi zote zilizopeleka majeshi katika Misheni za Umoja wa Mataifa unaofafanua stahiki mbalimbali za malipo kwa wanajeshi wanaoumia au kufariki wakati wa kutekeleza majukumu ya ulinzi wa amani. Waraka huo huzijulisha nchi wanachama zinazochangia vikosi, Maafisa wanadhimu na waangalizi wa amani stahiki ya malipo. Hivyo, siyo jukumu la nchi husika kuamua ilipwe fedha kiasi gani.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Misheni za SADC, hadi sasa hakuna Misheni inayomilikiwa na SADC pekee, bali iliyopo inaitwa Force International Brigade ambayo imeunganishwa na Misheni ya Umoja wa Mataifa nchini DRC ambayo taratibu za kulipa askari aliyeumia au kufariki bado inasimamiwa na Umoja wa Mataifa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa afisa au askari aliyeumia, utaratibu huo hufanyika kwa kuwasilisha nyaraka muhimu ambazo hutoa mwelekeo wa kiwango alichoumia ili alipwe kulingana na stahili.
Mheshimiwa Spika, kwa afisa au askari aliyefariki, Umoja wa Mataifa kwa sasa inalipa fidia ya dola za Kimarekani 70,000 kwa askari wa nchi yoyote aliyefariki akiwa anatekeleza majukumu ya ulinzi wa amani katika Misheni za Umoja wa Mataifa.