Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 24 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 202 2018-05-08

Name

Anna Joram Gidarya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANNA J. GIDARYA aliuliza:-
Mkoa wa Manyara ni moja kati ya maeneo yanayokubaliwa na changamoto ya migogoro ya ardhi katika wananchi wa Babati Vijijini hasa katika Vijiji vya Amayango, Gedamara na Hifadhi ya Tarangire kwa takribani miaka 11 sasa bila ufumbuzi wowote, migogoro hiyo imesababisha wananchi kukosa elimu, afya na uchumi kushuka ambapo majengo ya jamii yaliyopo ni madarasa manne, bweni moja, matundu 13 ya vyoo vya shule na jengo la zahanati na majengo haya yote yamejengwa kwa nguvu za wananchi.
• Je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza migogoro hiyo iliyodumu kwa muda mrefu na kurudisha maeneo ya wananchi yaliyochukuliwa na hifadhi?
• Endapo itabainika mipaka kati ya vijiji na hifadhi iliyooneshwa kwenye ramani ni batili. Je, Serikali husika iko tayari kuwalipa fidia wananchi wote walioathirika na migogoro hiyo kwa muda wa miaka 11?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Joram Gidarya, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uhakiki wa mpaka wa Hifadhi ya Taifa Tarangire na Vijiji vya Gedamar na Ayamango ulifanywa na wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi mwaka 2004 kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Namba 160 la mwaka 1970 lililoanzisha Hifadhi ya Taifa Tarangire. Baada ya uhakiki huo eneo hilo lilisimikwa vigingi (beacons) vya kuainisha mpaka wa hifadhi na vijiji husika ambao unafahamika kwa wananchi.
Mheshimiwa Spika, katika uhakiki huo ilibainika kuwa kaya 245 za vijiji vilivyotajwa hapo juu zilikuwa ndani ya eneo la Hifadhi ya Taifa Tarangire kimakosa. Ili kuwaondoa wananchi wa vijiji hivyo kutoka kwenye eneo la hifadhi, Serikali iliamua kuwalipa wananchi waliokuwa ndani ya eneo la hifadhi kifuta jasho kilichohusisha fidia ya mali, posho ya usumbufu, posho ya makazi na gharama za usafiri.
Mheshimiwa Spika, wananchi wa Vijiji vya Gedamar na Ayamango walilipwa jumla ya shilingi 137,845,592 tarehe 2 Februari, 2011 kupitia Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati. Baada ya malipo ya kifuta jasho wananchi wengi waliondoka isipokuwa kaya 42 ambazo ziliomba kupewa eneo mbadala la kuhamia. Halmashauri ya Wilaya ya Babati ilikubali kuwapatia wananchi hao eneo maeneo ya kuhamia kwenye shamba la Ufyomi lililopo Gallapo ambapo wananchi hao wameshapatiwa maeneo katika shamba hilo.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa hakuna mgogoro wa mpaka uliopo kati ya Vijiji vya Gedamar na Ayamango na Hifadhi ya Tarangire na mpaka uliopo kati ya hifadhi na vijiji hivyo ni sahihi.