Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 24 Energy and Minerals Wizara ya Madini 203 2018-05-08

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-
Je, ni lini Mgodi wa GGM utawasilisha bajeti yake ya kuhudumia jamii katika Baraza la Madiwani la Geita ili tuweze kuangalia kipaumbele chao na kuwapa vipaumbele vya Halmashauri ya Geita?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda sasa nijibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kifungu cha 105(1)(2) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na mabadiliko yake ya mwaka 2017 kinamtaka mmiliki wa leseni chini ya kifungu cha 7 cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 kuandaa Mpango wa Mwaka wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR). Mpango huo lazima ukubalike kwa pamoja na Mamlaka ya Serikali za Mtaa husika kwa kushauriana na Waziri anayehusika na Mamlaka za Serikali za Mitaa na Waziri anayehusika na Fedha.
Mheshimiwa Spika, mpango huo unapaswa kuzingatia masuala ya mazingira kijamii, kiuchumi na shughuli za tamaduni zilizopewa kipaumbele katika Mamlaka ya Serikali za Mtaa ya jamii inayozunguka mgodi.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 105(3), mmiliki wa leseni anapaswa kuwasilisha kwa Mamlaka ya Serikali za Mtaa husika mpango huo aliouandaa kwa ajili ya kufanyiwa tathmini na kupata idhini kutoka kwa Baraza la Madiwani wa Halmashauri. Aidha, kila halmashauri uliopo mgodi inapaswa kuandaa mwongozo wa utoaji wa huduma kwa jamii kwenye Halmashauri yao, kusimamia utekelezaji wake na kutoa elimu kwa wananchi wa wilaya husika juu ya huduma hizo.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa Mgodi wa GGM, kwa kushirikiana na halmashauri mbili za Geita Mji na Wilaya ya Geita, umeweza kutekeleza mchakato wa kuandaa mpango wake wa kusaidia jamii (CSR) kwa mwaka 2018 kama sheria inavyotaka. Mchakato huo umehusisha wataalam kutoka halmashauri zote mbili na wataalam wa Sekretarieti ya Mkoa.
Mheshimiwa Spika, mpango wa miradi iliyotambuliwa na halmashauri hizo kama vipaumbele umeshawasilishwa kwenye Mgodi wa GGM na umesharidhiwa na mgodi. Mgodi wa GGM unatarajia kutumia takribani shilingi bilioni 9.124 katika kutekeleza miradi iliyo chini ya mpango wa CSR. Kiasi cha shilingi bilioni moja kitatumika kutekeleza miradi katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, takribani shilingi bilioni 6.824 zitatumika kutekeleza miradi katika Halmashauri ya Mji wa Geita na takribani shilingi bilioni 1.3 zitatumika kutekeleza miradi katika Halmashauri za Bukombe, Chato na Mbogwe.
Baada ya taratibu zote kukamilika, mpango huo utawasilishwa katika Baraza la Madiwani ili uweze kuidhinishwa. Miradi iliyokubaliwa na wadau wote kwa mwaka 2018 itaanza kutekelezwa kabla ya mwezi Juni, 2018.