Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 37 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 313 2018-05-25

Name

Mbaraka Kitwana Dau

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Primary Question

MHE. MBARAKA K. DAU aliuliza:-
Kisiwa cha Mafia kinapata umeme kutoka kwenye jenereta kubwa ya TANESCO ambayo nayo inatumia mafuta mengi yenye gharama kubwa.
Je, ni lini Serikali itavusha umeme chini ya bahari (submarine cables) kutoka Nyamisati kwenda Kilindoni takribani kilometa 50?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, Mbunge wa Mafia, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imefanya tafiti za awali za kuona njia bora ya kuipatia Wilaya ya Mafia umeme wa uhakika na wa bei nafuu. Tafiti za awali zilizofanyika ni kuvusha umeme chini ya bahari (submarine cables) kutoka Nyamisati hadi Kilindoni na utafiti wa pili ni kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo mchanganyiko (hybrid) vya umeme jua, upepo na mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti hizi za awali zimeonesha kuwa gharama za kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo mchanganyiko ni nafuu zaidi na hivyo hatua za awali za utekelezaji wa mradi huu zimeshaanza. Uwezo wa mitambo hii ya kuzalisha umeme itakapokamilika inatarajiwa kuwa na megawati saba ikilinganishwa na uwezo wa megawati 3.68 zilizopo kwa sasa (megawati 2.18 zinamilikiwa na TANESCO na megawati 1.5 zinamilikiwa na kampuni binafsi ya Ng’omeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tayari TANESCO imeshapata eneo la mradi Wilayani Mafia kwa ajili ya kujenga mitambo ya kuzalisha umeme na inakamilisha taratibu za kumpata mshauri elekezi kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu utakaoainisha gharama halisi za utekelezaji wa mradi huo ambapo unatarajiwa kuanza kazi mwezi Juni, 2018 na kukamilika ndani ya miezi saba. Aidha, Benki ya Maendeleo ya Ufaransa imeonesha nia ya kufadhili mradi huo mara upembuzi yakinifu utakapokamilika.