Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 40 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 338 2018-05-30

Name

Abdulaziz Mohamed Abood

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Mjini

Primary Question

MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:-
Kuna mgogoro wa ardhi kati ya Jeshi la Wananchi kwenye mipaka katika Kata ya Kauzeni na Luhongo ambapo wananchi wanashindwa kufanya shughuli zao za maendeleo hasa kilimo, Jeshi linaweka mipaka na kuingiza ndani ya mashamba ya wananchi wakati miaka yote maeneo hayo yalikuwa nje ya mipaka ya Jeshi:-
• Je, ni lini Serikali itawarudishia wananchi maeneo yao ya kilimo?
• Je, kwa nini Serikali isichukue hatua kwa kuruhusu wananchi wamiliki maeneo hayo ambayo ni ya asili na Jeshi limewakuta wananchi katika eneo hilo?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdul-Aziz Mohamed Abood, Mbunge wa Morogoro Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi wa mgogoro wa mipaka ulishafanyika kwa kushirikiana na Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro. Hivyo, kimsingi Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania halina mgogoro na wananchi kwenye mipaka ya Kata za Kauzeni na Luhongo hasa baada ya upimaji mpya wa mwaka 2002 ambapo uliacha nje maeneo ya vijiji. Manung’uniko yaliyopo yanatokana na uamuzi wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kusitisha utaratibu wa kuwaruhusu kwa muda baadhi ya wananchi kulima mashamba ndani ya mipaka yake kwa sababu za kiulinzi na kiusalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yanayomilikiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania yapo kwa ajili ya ulinzi wa nchi na sehemu hizo zipo kimkakati kwa ajili ya usalama wa nchi. Serikali imetumia rasilimali nyingi za wananchi wa Tanzania kujenga miundombinu iliyopo kwenye eneo hilo. Hivyo, haitokuwa vema kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kuondoka katika maeneo yaliyochaguliwa kistratejia kwa ajili ya ulinzi. Ni vema wananchi waelimishwe juu ya jambo hili na nimwombe Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na wadau mbalimbali katika Halmashauri ya Mkoa kutoa elimu kwa wananchi. (Makofi)