Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 15 2019-01-30

Name

Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Primary Question

MHE. VEDASTO E. NGAMBALE aliuliza:-

Hifadhi ya Akiba ya Selous imekuwa ikihamisha alama za mipaka na kuchukua eneo la ardhi ya vijiji katika Jimbo la Kilwa Kaskazini bila ya kushirikisha Serikali ya Vijiji:-

Je, Serikali iko tayari kusimamia Mamlaka ya Hifadhi hiyo kurudisha alama za mipaka katika maeneo ya awali ili kuepusha mgogoro unaoweza kutokea?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Maliasili na Utalii inalo jukumu la kusimamia uhifadhi wa rasilimali za wanyamapori na misitu kwa kuzingatia uwepo wa mahusiano mazuri kati ya wananchi na maeneo yanayohifadhiwa. Jukumu hilo linatekelezwa kwa pamoja na mambo mengine kwa kutambua kulinda, kupitia upya na kuweka vigingi (beacons) katika mipaka ya Mapori ya Akiba, Hifadhi za Taifa, Hifadhi za Misitu na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iliagizwa kuweka vigingi kwenye mipaka ya hifadhi zote nchini kwa lengo la kuonesha mipaka kati ya hifadhi na vijiji ili kuepusha migogoro na uvamizi unaofanywa na wananchi na kusababisha malalamiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza maagizo haya, Wizara inafanya kazi ya kusimika vigingi kwenye mipaka ya mapori yote ya akiba likiwemo Pori la Akiba la Selous. Aidha, zoezi la upitiaji, uhakiki na usimikaji wa vigingi katika Pori la Akiba la Selou upande wa Kilwa Kaskazini limefanyika katika Kijiji cha Namatewa. Zoezi hili limefanyika kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya pamoja na Uongozi wa Vijiji kwenye maeneo hayo. Kazi ilifanyika kwa kutumia Tangazo la Serikali Na. 275 la Mwaka 1974 lililoanzisha pori hilo na ramani za vijiji husika kwa kushirikiana na Wapima wa Ardhi wa Wilaya zinazopakana na mapori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya mpaka wa Pori la Akiba la Selous ambalo halijasimikwa vigingi upande wa Kilwa Kaskazini ni katika Vijiji vya Mtepera na Zinga Kibaoni. Hii ni kutokana na wananchi wa vijiji husika kutotambua ukomo wa mpaka kwa mujibu wa ramani za vijiji vyao wakidai eneo linalosalia ni la kijiji na siyo la hifadhi. Kwa mantiki hiyo, hakuna uhamishaji wa alama za mpaka uliofanywa kwa nia ya kuchukua eneo la ardhi la kijiji karibu na Pori la Akiba la Selous.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara zingine sita, imeelekezwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia upya maeneo yenye ubishani na migogoro ikiwa ni pamoja na vijiji na kuangalia mipaka ili kuondoa migogoro hiyo. Kwa sasa Wizara inaendelea kuweka utaratibu mzuri wa namna ya utekelezaji wa agizo hilo.