Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 3 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 28 2019-01-31

Name

Catherine Valentine Magige

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CATHERINE V. MAGIGE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawalipa wafanyakazi 545 wa KILTEX – Arusha ambao bado wanadai pensheni toka kiwanda hicho kilipofungwa baada ya Mwajiri wao kutowasilisha michango yao kwenye Mfuko wa Kijamii wa PPF?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Nguo cha KILTEX, kilisimamisha shughuli za uzalishaji mwaka 1994 na kuwekwa chini ya ufilisi na PSRC mwaka 1995, kutokana na tatizo la ukosefu wa mtaji na malimbikizo ya madeni. Kwa mujibu wa ripoti ya Mfilisi, kiwanda kilishindwa kutekeleza takwa la kisheria la kuwasilisha mchango wa mwajiri na waajiriwa kwenye Mfuko wa Pensheni wa PPF kati ya mwaka 1986 na 1994 na hivyo kusababisha PPF kushindwa kuandaa malipo ya mafao ya wafanyakazi kulingana na matakwa ya kisheria mara baada ya kiwanda kufungwa na kufilisiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kumbukumbu na nyaraka za ufilisi zilizopo, taratibu za ufilisi zilikamilika na wafanyakazi wa KILTEX walilipwa stahili zao. Hata hivyo, baadhi ya wafanyakazi walilipwa mafao ya kiinua mgongo kwa mkupuo na wengine walirejeshewa michango yao kwa kadri walivyochangia. Utaratibu huu wa malipo ulifanyika baada ya Mfilisi kushindwa kulipa riba, adhabu na malimbikizo ya michango kwenye Mfuko wa Pensheni wa PPF. Uamuzi huo ulifikia kutokana na ukweli kwamba mauzo ya mali za kiwanda yalikuwa kidogo ikilinganishwa na jumla ya madai na gharama halisi za ufilisi.

Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba watumishi wa Kiwanda cha KILTEX walilipwa stahili zao kwa mujibu wa Sheria ya Makampuni Na. 46 ya mwaka 1931 ambayo ilitumika kufilisi kiwanda mwaka 1995. Kwa mujibu wa sheria hiyo, Mfilisi alitakiwa kuuza mali za kiwanda na kutumia fedha za mauzo kulipa madai mbalimbali ikiwa ni pamoja na stahili za watumishi ndani ya muda maalum kulingana na tangazo la ufilisi. Kufuatia tangazo la Mfilisi kwenye vyombo vya habari, wadai waliwasilisha madai yao na Mfilisi alilipa madeni hayo kulingana na fedha mauzo zilizopatikana.