Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 8 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 86 2019-02-06

Name

George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-

Waheshimiwa Madiwani wana majukumu mengi ya kufanya katika kata zao; na posho wanayolipwa kwa mwezi hailingani kabisa na majukumu yao na ni ndogo sana:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza posho ya Waheshimiwa Madiwani?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiongeza posho na maslahi ya Madiwani nchini kwa awamu kulingana na uwezo wa halmashauri kukusanya mapato ya ndani. Serikali ilipandisha posho za mwezi za Madiwani kutosha Sh.120,000 kwa mwaka 2012/2013 hadi shilingi 250,000 kupitia Waraka wa tarehe 16, Agosti, 2012 na posho za madaraka kwa Wenyeviti wa Halmashauri na Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Halmashauri. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2014/2015 kupitia Waraka wa Waziri mwenye dhamana na Serikali za Mitaa wa Tarehe 23, Desemba, 2014, Serikali ilipandisha posho za Madiwani kutoka Sh.250,000 hadi Sh.350,000 kwa mwezi kwa Madiwani na Sh.350,000 hadi Sh.400,000 kwa mwezi kwa Wenyeviti wa Halmashauri na Mameya pamoja na posho nyingine kama ilivyoainishwa kwenye Waraka wa tarehe 26, Novemba, 2007.

Mheshimiwa Naibu Spika, ongezeko la posho na maslahi ya Madiwani inatokana na halmashauri kuongeza makusanyo ya mapato ya ndani. Hivyo, natoa wito kwa halmashauri kuimarisha makusanyo ya mapato ya ndani ya halmashauri ili kujenga uwezo wa ndani na kulipa posho hizo kwa Madiwani.