Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 103 2019-02-07

Name

Lathifah Hassan Chande

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LATHIFA H. CHANDE aliuliza:-

Wananchi wa Mkoa wa Lindi wanakabiliwa na changamoto kubwa ya hali duni ya huduma za afya kwa kuwa na uchache wa Wauguzi, Madaktari wa kawaida na wa akina mama na uhaba wa vifaa na dawa, lakini pia Vituo vya Afya na Zahanati hazitoshi:-

(a) Je, ni lini Serikali itaongeza Wauguzi, vifaa tiba na dawa katika Hospitali ya Wilaya ya Liwale?

(b) Hospitali ya Ruangwa kwa kipindi kirefu imekuwa haina huduma ya X-Ray hali inayowalazimu wananchi wa Wilaya ya Ruangwa kufuata huduma hiyo Lindi: Je, ni lini Serikali itatatua tatizo hilo?

(c) Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa nyumba za Wauguzi na Mganga Mkuu katika Zahanati ya Mtawango katika Kata ya Mtawango, Liwale?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali ya Mheshimiwa Lathifa Hasan Chande, Mbunge wa Viti Maalum, Lenye Sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliajiri watumishi wa kada mbalimbali za Afya 6,180. Kati ya hao, 89 walipangwa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale. Mwaka wa fedha 2017/2018 na 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Liwale imepokea jumla ya shilingi milioni 345.5 kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi. Aidha, upatikanaji wa dawa muhimu katika vituo vyote 242 vya kutolea huduma za afya Mkoani Lindi kuanzia Januari hadi Desemba, 2018 ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Liwale ulikuwa ni kwa zaidi ya asilimia 91.9.

(b) Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Wilaya ya Ruangwa ilifungiwa mashine ya X-Ray mwaka 2015 ambapo mpaka Desemba, 2018 Wagonjwa 7,250 wamehudumiwa. Ni kweli kuna wakati mashine hii ilipata hitilafu na ikashindwa kufanya kazi, lakini hitilafu hiyo ilirekebishwa na mashine ya X-Ray inaendelea kutoa huduma. Mpango wa Serikali ni kuipatia hospitali hii X-Ray ya kisasa.

(c) Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi wa Zahanati pamoja na nyumba za Watumishi Mtawango ulikuwa ni mradi unaofadhiliwa na TASAF katika mwaka wa fedha 2015/2016 kujenga nyumba mbili kwa moja (two in one), ambapo fedha zilizopangwa na kutumika ni shilingi milioni 27. Hata hivyo, fedha hizo hazikutosheleza kumalizia ujenzi wa nyumba. Hivyo, Halmashauri imepanga kutenga shilingi milioni 10 katika bajeti ya mapato ya ndani ya mwaka 2019/ 2020 ili kukamilisha ujenzi wa nyumba ya Muuguzi na Mganga katika Zahanati ya Mtawango.