Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 104 2019-02-07

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Primary Question

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:-

Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 2 ya Mwaka 2018 yamemwondoa Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika kushitaki kesi zote za jinai nchini, lakini Katiba ya Jamhuri ya Muungano inamtambua Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika mambo ya Muungano:-

Je, kumwondoa moja kwa moja Mwanasheria Mkuu wa Serikali hakuwezi kuathiri makosa ya jinai ya uhaini yanayoweza kutokea Zanzibar kukwama kwa kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka hana mamlaka kwa mujibu wa Katiba na mambo ya Muungano kushitaki Zanzibar?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ibara ya 59(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Sheria ya Ofisi ya Mashitaka, Sura ya 430, masuala ya ufunguaji, uendeshaji na usimamizi wa mashitaka ya jinai nchini yako chini ya Mkurugenzi wa Mashitaka na siyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Kwa upande wa Zanzibar, masuala hayo yanaongozwa na Ibara ya 56(a) ya Katiba ya Zanzibar na Sheria ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka Na. 2 ya Mwaka 2010. Katika Katiba zote mbili na sheria zake, mamlaka ya mwisho ya kufungua, kuendesha na kusimamia mashitaka ya jinai ni ya Mkurugenzi wa Mashitaka. Hivyo, masuala ya jinai siyo suala la Muungano.

Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kuwa tarehe 13 Februari, 2018 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alifanya mabadiliko ya muundo wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ambapo pamoja na mambo mengine alianzisha Ofisi Huru ya Taifa ya Mashitaka. Ili kuendana na mabadiliko hayo ya muundo, yalifanyika kurekebisha kwenye Sheria ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (Utekelezaji wa Majukumu) Sura ya 268 kwa kukifuta Kifungu cha 8 na kukibadilisha kupitia Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 2 ya Mwaka 2018.

Mheshimiwa Spika, marekebisho hayo yamemwondoa Mkurugenzi wa Mashitaka na iliyokuwa Division ya Mashitaka kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Hivyo, mabadiliko hayo hayajaathiri kwa namna yoyote ufunguaji, uendeshaji na usimamizi wa mashauri ya jinai nchini. Bado kwa mujibu wa Ibara ya 59(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Mkurugenzi wa Mashitaka anaendelea kuwa na mamlaka ya juu ya mashauri yote ya jinai nchini.

Mheshimiwa Spika, makosa yote ya jinai yanayotokea katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yanaendelea kushughulikiwa kwa mujibu wa sheria zilizopo na hayawezi kukwama kwa kuwa kuna mifumo mizuri ya kikatiba, kisheria na kitaasisi ya kuyashughulikia.